Anulado
Hospitali ya Al-Shifa
19 de Dezembro de 2023
Bodi imebatilisha uamuzi wa kwanza wa Meta wa kuondoa maudhui hayo kutoka kwenye Instagram. Imegundua kuwa kurudisha maudhui kwenye jukwaa, kwa kutumia skrini ya onyo ya “alamisha kuwa ya kutisha”, kunalingana na sera za maudhui ya Meta, maadili na majukumu ya kulinda haki za binadamu.
Wiki zinazofuata baada ya kuchapishwa kwa uamuzi huu, tutapakia tafsiri ya Kiebrania hapa na tafsiri ya Kiarabu itapatikana kupitia kichupo cha ‘lugha’ kinachopatikana katika menyu iliyo juu ya skrini hii.
לקריאת החלטה זו בעברית יש ללחוץ כאן.
1. Muhtasari
Kesi hii inahusisha video yenye masuala makali ya kihisia ya baada ya shambulio kwenye au karibu na hospitali ya Al-Shifa mjini Gaza wakati wa mashambulizi ya ardhini ya Israeli, na manukuu yanayokashifu shambulio hilo. Mifumo otomatiki ya Meta iliondoa chapisho hilo kwa kukiuka Viwango vyake vya Jumuiya kuhusu Maudhui ya Vurugu na Michoro. Baada ya kukosa kufanikiwa kupinga uamuzi kwa Meta, mtumiaji alikata rufaa kwa Bodi ya Usimamizi. Baada ya Bodi kutambua kesi hii, Meta ilibatilisha uamuzi wake na kurejesha maudhui kwa kuweka skrini ya onyo. Bodi inashikilia kuwa uamuzi wa kwanza wa kuondoa maudhui haukutii sera za maudhui za Meta au wajibu wa kampuni hiyo wa kulinda haki za binadamu. Bodi imeidhinisha uamuzi wa kurejesha maudhui kwa kutumia skrini ya onyo lakini haikubaliani na ushushaji unaohusishwa na maudhui hayo kuzuiwa katika mapendekezo. Kesi hii, pamoja na Mateka Waliotekwa Nyara Kutoka Israeli ( 2023-050-FB-UA), ndizo kesi za kwanza ambazo Bodi iliamua chini ya taratibu zake za ukaguzi wa haraka.
2. Muktadha na Majibu ya Meta
Mnamo Oktoba 7, 2023, Hamas, shirika la Safu ya 1 chini ya Kiwango cha Jumuiya ya Meta kuhusu Mashirika na Watu Binafsi Hatari, liliongoza mashambulizi ya kigaidi dhidi ya Israel kutoka Gaza ambayo yalisababisha vifo vya takriban watu 1,200 na kusababisha takriban watu 240 kuchukuliwa mateka ( Wizara ya Mambo ya Nje, Serikali ya Israel). Israel ilianza mara moja kampeni ya kijeshi huko Gaza ili kujibu mashambulizi hayo. Hatua ya kijeshi ya Israel imeua zaidi ya watu 18,000 huko Gaza kufikia katikati ya mwezi Desemba 2023 (Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kuratibu Masuala ya Binadamu, ikichukua data kutoka kwa Wizara ya Afya huko Gaza), katika mgogoro ambapo pande zote mbili zimeshutumiwa kwa kukiuka sheria za kimataifa. Mashambulio yote ya kigaidi na hatua za kijeshi za Israel zilizofuata zimekuwa mada ya utangazaji, mijadala, uchunguzi na mabishano makubwa duniani kote, ambayo mengi yamefanyika kwenye majukwaa ya mitandao ya kijamii, zikiwemo Instagram na Facebook.
Mara moja Meta ilibainisha matukio ya Oktoba 7 kuwa shambulio la kigaidi chini ya sera yake ya Mashirika na Watu Hatari. Chini ya Viwango vyake vya Jumuiya, hii inamaanisha kuwa Meta ingeondoa maudhui yoyote kwenye majukwaa yake ambayo “yanasifu, kuunga mkono kwa kiasi kikubwa au kuwakilisha” mashambulio ya Oktoba 7 au wahalifu wanaoshukiwa kuyatekeleza.
Kutokana na ongezeko la kipekee la maudhui ya vurugu na michoro yanayochapishwa kwenye majukwaa yake kufuatia mashambulizi ya kigaidi na majibu ya kijeshi, Meta iliweka hatua kadhaa hatua kadhaa za muda mfupi, ikiwa ni pamoja na kupunguza upeo wa uaminifu kwa mifumo yake otomatiki ya kuainisha Maudhui ya Vurugu na Michoro (kiainishaji) ili kutambua na kuondoa maudhui. Meta ilifahamisha Bodi kwamba hatua hizi zinatumika kwa maudhui yanayotoka Israel na Gaza katika lugha zote. Mabadiliko ya viainishaji hivi yaliongeza uondoaji wa kiotomatiki wa maudhui ambapo kulikuwa na alama ya chini ya kuamini maudhui yanayokiuka sera za Meta. Kwa maneno mengine, Meta ilitumia zana zake za kiotomatiki kwa kina zaidi ili kuondoa maudhui ambayo yanaweza kukiuka sera zake. Meta ilifanya hivi ili kutanguliza thamani yake ya usalama, huku maudhui mengi yakiondolewa kuliko ambavyo ingetokea chini ya kiwango cha juu cha imani kilichowekwa kabla ya tarehe 7 Oktoba. Ingawa hii ilipunguza uwezekano kwamba Meta itashindwa kuondoa maudhui yanayokiuka ambayo yanaweza kukosa kutambuliwa au ambapo uwezo wa ukaguzi wa binadamu ulikuwa mdogo, pia iliongeza uwezekano wa Meta kuondoa kimakosa maudhui yasiyokiuka yanayohusiana na mgogoro.
Wakati timu za ukaguzi ilitathmini video na kubaini kuwa zinakiuka sera zake za Maudhui ya Vurugu na Michoro, Vurugu na Uchochezi na Mashirika na Watu Binafsi Hatari, Meta ilitegemea hifadhi za Huduma ya Kulinganisha Midia ili kuondoa video zinazolingana kiotomatiki. Mbinu hii iliibua wasiwasi wa utekelezaji kupita kiasi, ikiwemo watu wanaokabiliwa na vizuizi vya au akaunti zao kusimamishwa kufuatia ukiukaji mwingi wa sera za maudhui za Meta (wakati fulani hujulikana kama “jela ya Facebook”). Ili kupunguza wasiwasi huo, Meta ilizuia “maonyo” ambayo kwa kawaida yangeambatana na uondoaji wa maudhui unaofanyika kiotomatiki kulingana na hifadhi za Huduma ya Kulinganisha Midia (kama Meta ilivyotangaza kwenye chapisho lake la chumba cha habari).
Mabadiliko ya Meta katika kiwango cha kuamini kiainishaji na sera yake ya onyo yanahusu tu mzozo wa Israel-Gaza na yananuiwa kuwa ya muda mfupi. Kufikia tarehe 11 Desemba 2023, Meta ilikuwa haijarejesha viwango vya imani hadi viwango vya kabla ya Oktoba 7.
3. Ufafanuzi wa Kesi
Maudhui katika kesi hii yanahusisha video iliyochapishwa kwenye Instagram katika wiki ya pili ya Novemba, inayoonyesha kile kinachoonekana kuwa matokeo ya shambulio kwenye au karibu na Hospitali ya Al-Shifa katika Jiji la Gaza wakati wa shambulio la ardhini kaskazini mwa Ukanda wa Gaza. Chapisho la Instagram katika kesi hii linaonyesha watu, ikiwa ni pamoja na watoto, wakilala chini wakiwa wamekufa, au kujeruhiwa na kulia. Mtoto mmoja anaonekana kuwa amekufa, akiwa na jeraha baya sana kichwani. Manukuu haya katika lugha ya Kiarabu na Kiingereza yaliyo chini ya video hii yanasema kuwa hospitali hiyo imelengwa na “ukaaji wa unyakuzi,” ikirejelea jeshi la Israeli, na linaweka lebo kwenye haki za binadamu na mashirika ya habari.
Viwango vya Jumuiya ya Meta vya Maudhui ya Vurugu na Michoro, ambavyo vinatumika kwa maudhui kwenye Facebook na Instagram, vimepiga marufuku “[v]ideo za watu au miili ya watu waliokufa katika mazingira yasiyo ya kimatibabu ikiwa zinaonyesha … [v]iungo dhahiri vya ndani.” Kufikia wakati wa kuchapishwa, sera hii iliruhusu “picha zinazoonyesha kifo cha vurugu cha mtu au watu kupitia ajali au mauwaji,” ilimradi maudhui kama hayo yalionyeshwa baada ya kuonyesha skrini ya onyo ambayo “imetiwa alama kuwa inatatiza” na yalikuwa yanaweza kuonekana na watu wenye umri zaidi ya miaka 18 pekee. Kanuni hii ilisasishwa tarehe 29 Novemba, baada ya maudhui husika katika kesi hii kurejeshwa, ili kubainisha kuwa kanuni hii inatumika katika “wakati wa kifo au matokeo” na vilevile picha ya “mtu anayepitia tukio la kutishia maisha.”
Mifumo otomatiki ya Meta iliondoa maudhui katika kesi hii kwa kukiuka Viwango vya Jumuiya vya Maudhui ya Vurugu na Michoro. Rufaa ya mtumiaji dhidi ya uamuzi huu ulikataliwa kiotomatiki kwa sababu viainishaji vya Meta viliashiria “kiwango cha juu cha kuamini” kuwa maudhui hayo yalikuwa ya ukiukaji. Kisha mtumiaji akakata rufaa dhidi ya uamuzi wa Meta kwa Bodi ya Usimamizi.
Kufuatia hatua ya Bodi ya kuteua kesi hii, Meta ilisema kuwa haingeweza kubaini kikamilifu kuwa video ilionyesha viungo dhihiri vya ndani ya mwili. Kwa hivyo Meta ilihitimisha kuwa haikupaswa kuondoa maudhui haya, ingawa yalikuwa “yamekaribia” kuwa ya ukiukaji. Meta iliendelea kueleza kuwa hata kama viungo vya ndani vilikuwa vikionekana, chapisho hilo lingepaswa kuachwa likiwa na skrini ya onyo ya “weka alama kuwa inatatiza” kwa sababu lilishirikiwa ili kutoa uhamasisho. Kampuni hiyo ilisisitiza kuwa, kulingana na utaratibu wa sera ya Maudhui ya Vurugu na Michoro, maudhui kama hayo yanaruhusiwa kushirikiwa ili kutoa uhamasisho “kuhusu masuala muhimu kama vile ukiukaji wa haki za binadamu, migogoro ya kivita au vitendo vya ugaidi.”
Kwa hivyo Meta ilibatilisha uamuzi wake wa kwanza na kurejesha maudhui hayo yakiwa na skrini ya onyo. Skrini ya onyo hufahamisha watumiaji kuwa maudhui yanaweza kuwa ya kutatiza. Watumiaji ambao ni watu wazima wanaweza kubofya ili kuona chapisho, lakini Meta huondoa machapisho haya kwenye milisho ya watumiaji wa Instagram ambao umri wao ni chini ya miaka 18 na pia huyaondoa kwenye mapendekezo kwa watumiaji wa Instagram ambao ni watu wazima. Meta pia iliongeza tukio tofauti la video ile moja kwenye hifadhi ya Huduma ya Kulinganisha Maudhui, ili video nyingine zinazofanana na hii ziweze kufuatiliwa kiotomatiki na kuwekewa skrini ya onyo na zingeweza kuonekana kwa watu wenye umri wa zaidi ya miaka 18 pekee.
4. Uthibitishaji wa Ukaguzi wa Haraka
Sheria ndogo za Bodi ya Usimamizi zinahalalisha ukaguzi wa haraka katika “hali za kipekee, ikiwa ni pamoja na wakati kuna uwezekano wa maudhui kusababisha madhara halisi ya dharura,” na maamuzi ni ya lazima katika Meta (Mkataba, Kifungu cha 3, sehemu ya 7.2; Sheria ndogo, Kifungu cha 2, sehemu ya 2.1.2). Mchakato wa haraka unazuia kiwango cha utafiti wa kina, mashauriano ya nje au maoni ya umma ambayo yangetolewa katika kesi zilizopitiwa kwa muda wa kawaida. Kesi hiyo huamuliwa kulingana na taarifa zinazopatikana kwa Bodi wakati wa mashauriano na huamuliwa na jopo la wanachama watano bila kura kamili ya Bodi.
Bodi ya Usimamizi ilichagua kesi hii na kesi nyingine moja, Mateka Waliotekwa Nyara Kutoka Israeli (2023-050-FB-UA) kwa sababu ya umuhimu wa uhuru wa kujieleza katika hali ya migogoro, ambayo imekuwa hatarini katika muktadha wa mgogoro wa Israel na Hamas. Kesi zote mbili ni uwakilishi wa aina za rufaa ambazo watumiaji katika eneo hilo wamekuwa wakiwasilisha kwenye Bodi tangu shambulio la Oktoba 7 na hatua ya kijeshi ya Israeli iliyofuata. Kesi zote ziko ndani ya kipaumbele cha hali ya mgogoro na mzozo katika Bodi ya Usimamizi. Maamuzi ya Meta katika kesi zote mbili yanakidhi kiwango cha “matokeo ya dharura ya ulimwengu halisi” ili kuhalalisha ukaguzi wa haraka, na kwa hivyo Bodi na Meta zilikubali kuendelea chini ya taratibu za Bodi zilizoharakishwa.
Katika mawasilisho yake kwa Bodi, Meta ilitambua kuwa “uamuzi kuhusu jinsi ya kushughulikia maudhui haya ni mgumu na unahusisha ushindani wa thamani na usawazishaji” ikikaribisha maoni ya Bodi kuhusu suala hili.
5. Mawasilisho ya Mtumiaji
Mchapishaji wa chapisho alisema kwenye rufaa yake kwa Bodi kuwa hakuchochea vurugu yoyote, lakini alishiriki maudhui hayo kuonyesha hali ya kuteseka kwa Wapalestina, ikijumuisha watoto. Mtumiaji aliongeza kuwa kuondolewa kwa maudhui hayo kulikuwa ni uonevu dhidi ya mateso ya Wapalestina. Mtumiaji aliarifiwa kuhusu ukaguzi wa Bodi wa rufaa yao.
6. Uamuzi
Ingawa wanachama wa Bodi hawajakubaliana kuhusu mwitikio wa jeshi la Israeli na sababu zilizotolewa, wanakubaliana kwa kauli moja kuhusu umuhimu wa Meta kuheshimu haki ya kujieleza huru na haki nyingine za binadamu za watu wote walioathiriwa na matukio haya na uwezo wao wa kuwasiliana katika janga hili.
Bodi imebatilisha uamuzi wa kwanza wa Meta wa kuondoa maudhui hayo kutoka kwenye Instagram. Imegundua kuwa kurudisha maudhui kwenye jukwaa, kwa kutumia skrini ya onyo ya “alamisha kuwa ya kutisha”, kunalingana na sera za maudhui ya Meta, maadili na majukumu ya kulinda haki za binadamu. Hata hivyo, Bodi pia inahitimisha kuwa Meta wa kushusha maudhui yaliyorejeshwa, kwa namna ya kutengwa kuweza kupendekezwa, hakulingani na majukumu ya kampuni ya kuheshimu uhuru wa kujieleza.
6.1 Utiifu wa Sera za Maudhui za Meta
Bodi inakubaliana na Meta kwamba ni vigumu kubaini iwapo video katika kesi hii inaonyesha “[s]ehemu dhahiri za ndani ya mwili.” Kutokana na muktadha wa kesi hii, ambapo kuna thamani ya kipekee ya maslahi ya umma katika kulinda ufikiaji wa taarifa na kutoa njia za kutoa uhamasisho kuhusu athari ya mgogoro, maudhui ambayo “yanakaribia” kukiuka sera ya Maudhui ya Vurugu na Michoro hayapaswi kuondolewa. Kwa kuwa maudhui yanajumuisha picha zinazoonyesha kifo cha vurugu cha mtu, yanayoonyesha jeraha la kichwa chenye damu, Meta inapaswa kuweka skrini ya onyo na kufanya ipatikane tu kwa watu wenye umri wa zaidi ya miaka 18 kulingana na sera zake.
Bodi pia inakubaliana na ubainisho wa baadaye wa Meta kwamba hata ikiwa video hii ilijumuisha viungo dhahiri vya ndani, lugha ya chapisho ya kukashifu au kutoa uhamasisho kuhusu vurugu pia inamaanisha kuwa lilipaswa kuachwa likiwa na skrini ya onyo inayosema “weka alama kuwa inatatiza” na lisipatikane kwa watumiaji wenye umri wa chini ya miaka 18. Viwango vya Jumuiya havitoi skrini za onyo kuhusiana na sera inayotumika (“[v]ideo za watu au miili ya watu waliokufa katika mazingira ya matibabu ikiwa yanaonyesha […] [v]iungo vya dhahiri vya ndani”). Katika kesi ya Video ya Kuogofya ya Sudan, Bodi ilieleza kuwa Meta ilishauri wakaguzi kufuatilia kusudi la sera zake za “usichapishe”. Sababu ya msingi inasema kwamba “[k]atika muktadha wa mijadala kuhusu masuala muhimu kama vile ukiukwaji wa haki za binadamu, migogoro ya silaha au vitendo vya ugaidi, tunaruhusu maudhui ya waziwazi (yaliyo na vikwazo fulani) kulaani na kuongeza ufahamu kuhusu hali hizi.” Kanuni ya Viwango vya Jumuiya, hata hivyo, imepiga marufuku video zote zinazoonyesha “viungo dhahiri vya ndani” katika muktadha usio wa kimatibabu, bila kuwapa wakaguzi chaguo la kuweka skrini ya onyo ambapo kighairi cha utaratibu wa sera hutumika. Mifumo otomatiki ya Meta haonekani kusawazishwa ili kuweka skrini za onyo kwenye video zinazoonyesha maudhui ya michoro ambapo kuna muktadha unaokashifu au kutoa uhamasisho kuhusu vurugu, Pia si wazi kwamba pale ambapo muktadha huu upo, viainishaji vinavyotumika vingeweza kutuma maudhui hayo kwa wakaguzi binadamu kwa ajili ya tathmini za ziada.
6.2 Utiifu wa Wajibu wa Haki za Binadamu wa Meta
Kulingana na wajibu wake wa haki za binadamu, uratibu wa Meta wa maudhui ya vurugu na michoro lazima uheshimu haki ya uhuru wa kujieleza, ambayo ni pamoja uhuru wa kutafuta, kupokea na kutoa taarifa (Kifungu cha 19, aya ya 2, Mkataba wa Kimataifa juu ya Haki za Kiraia na Kisiasa ( ICCPR)). Kama Bodi ilivyosema katika kesi ya Video ya Wafungwa wa Kivita wa Armenia, ulinzi wa uhuru wa kujieleza chini ya Kifungu cha 19 cha Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa (ICCPR) unaendelea kutumika wakati wa migogoro ya silaha, na unapaswa kuendelea kujulisha wajibu wa haki za binadamu wa Meta, pamoja na kanuni za kuimarisha na zinazotimizana za sheria za kibinadamu za kimataifa ambazo zinatumika wakati wa migogoro hiyo.” Kanuni za Mwongozo za Umoja wa Mataifa kuhusu Biashara na Haki za Kibinadamu huweka wajibu mkubwa kwa biashara zinazofanya kazi katika mazingira ya migogoro (“Biashara, haki za binadamu na maeneo yaliyoathiriwa na migogoro: kuelekea hatua zilizoimarishwa,” A/75/212).
Bodi imesisitiza katika kesi za awali kuwa majukwaa ya mitandao ya kijamii kama vile Facebook na Instagram ni njia muhimu ya kupitisha taarifa za wakati halisi kuhusu matukio ya vurugu, ikiwa ni pamoja na kuripoti habari (tazama mfano Kutajwa kwa Taliban katika Kuripoti Habari). Yanachukua nafasi muhimu haswa katika miktadha ya migogoro ya kivita, hususan pale ambapo wanahabari wanadhibitiwa. Zaidi ya hayo, maudhui yanayoonyesha mashambulizi vya vurugu na dhuluma za haki za binadamu ni za maslahi makubwa ya umma (Tazama Video ya Michoro ya Sudan).
Ambapo serikali imeweka vikwazo dhidi ya usemi, chini ya sheria ya kimaitaifa ya haki za binadamu, vikwazo hivyo lazima vitimize masharti ya kutii sheria, lengo halali na umuhimu na ulinganifu (Kifungu cha 19, aya ya 3 ya ICCPR). Masharti haya mara nyingi huitwa “jaribio la sehemu tatu.” Bodi hutumia mfumo huu kutafsiri ahadi za hiari za haki za binadamu za Meta, kuhusiana na uamuzi wa maudhui ya mtu binafsi unaokaguliwa na kile kinachosemwa na Meta kuhusu usimamizi wa maudhui. Kwa kufanya hivyo, Bodi hujaribu kuwa makini na jinsi haki hizo zinavyoweza kuwa tofauti kama zinavyotumika kwa kampuni ya kibinafsi ya mitandao ya kijamii kuliko inavyotumika kwa serikali. Hata hivyo, kama vile Mjumbe Maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu uhuru wa kujieleza alivyosema kwamba ingawa kampuni hazina wajibu wa serikali, “aina ya athari zao huzihitaji kutathmini aina sawa ya maswali kuhusu kulinda haki za kujieleza huru” ( ripoti ya A/74/486, aya ya 41).
Uhalali unahitaji kwamba kizuizi chochote cha uhuru wa kujieleza kinapaswa kupatikana na kwa njia wazi kabisa ili kutoa mwongozo kuhusu kile kinachoruhusiwa na kisichoruhusiwa. Awali Bodi ilionyesha wasiwasi kuwa kanuni za Viwango vya Jumuiya kuhusu Maudhui ya Vurugu na Michoro haviambatani kikamilifu na utaratibu wa sera, unaobainisha malengo ya sera (Tazama Video ya Michoro ya Sudan na Video Baada ya Shambulio la Kanisa nchini Naijeria). Bodi inasisitiza umuhimu wa mapendekezo nambari 1 na nambari 2 katika kesi ya Video ya Michoro ya Sudan, ambayo yalitoa mwito kwa Meta kufanya marekebisho kwenye Viwango vyake vya Jumuiya kuhusu Maudhui ya Vurugu na Michoro ili kuruhusu video za watu au miili ya watu waliokufa zinaposhirikiwa kwa madhumuni ya kutoa uhamasisho au kurekodi visa vya dhuluma za haki za binadamu (kesi hiyo ilihusisha viungo dhahiri vya mwili vilivyokatwa.) Meta imefanya mchakato wa uundaji wa sera ili kuitikia mapendekezo haya na inanuia kuripoti kuhusu maendeleo yake katika taarifa yake ijayo ya robo mwaka kwa Bodi. Kwa mtazamo wa Bodi, pendekezo hili linapaswa kutumika kwa kanuni za video zinazoonyesha viungo dhahiri vya ndani, na haswa kutoa skrini za onyo kama hatua ya utekelezaji pale ambapo vighairi vya utoaji uhamasisho (ikijumuisha kuripoti ukweli) na kukashifu vinatumiwa.
Chini ya Kifungu cha 19, aya ya 3 ya ICCPR, usemi unaweza kuzuiwa kwa orodha iliyofafanuliwa na yenye vizuizi ya sababu. Awali Bodi iligundua kuwa sera ya Maudhui ya Vurugu na Michoro ina lengo halali la kulinda haki za wengine, ikijumuisha haki za mtu binafsi aliyeonyeshwa (Angalia Video ya Michoro ya Sudan na Video Baada ya Shambulio Kanisani Nchini Naijeria). Kesi ya sasa inaonyesha, vilevile, kuwa kudhibiti ufikiaji wa maudhui kwa watu wenye umri wa chini ya miaka 18 kulitimiza lengo halali la kulinda haki ya afya ya watoto wadogo (Azimio kuhusu Haki za Mtoto, Kifungu cha 24).
Kanuni ya umuhimu na usawa inatoa vizuizi vyovyote vya uhuru wa kujieleza “lazima viwe vinafaa ili kufanikisha kazi yao ya ulinzi; lazima viwe ni vyombo vya ukali wa chini zaidi kati ya vile vinavyoweza kufikia lengo lao la ulinzi; [na] lazima viwe na usawa na mapendeleo ya kulindwa” ( Maoni ya Jumla Nambari 34, aya ya 34).
Awali Bodi iligundua kuhusiana na maudhui ya vurugu na michoro kwamba skrini ya onyo “haiweki wajibu usiofaa kwa wale ambao wangependa kuona maudhui huku ikifahamisha wengine kuhusu hali ya maudhui hayo na kuwaruhusu kuamua iwapo watayaona au la” (Tazama Video ya Kuogofya ya Sudan). Skrini za onyo huzuia watumiaji dhidi ya kutazama maudhui ambayo yanaweza kuwa ya kutatiza bila kukusudia. Haki za waathiriwa zinaendelea kulinda na sera ya Meta ya kuondoa video na picha zinazoonyesha kifo cha vurugu cha mtu (au matokeo yake ya papo hapo) wakati mwanafamilia ameomba hili. Maudhui kwenye kesi hii yanaweza kutofautishwa na yale yaliyo wenye kesi ya Shairi la Urusi, ambayo yalionyesha picha tuli ya mwili uliolala ardhini kwa mbali, ambapo uso wa mwathiriwa haukuwa ukionekana, na ambapo hakuna viashiria vya wazi vya vurugu. Kuweka skrini ya onyo kwenye kesi hiyo hakukuambatana na mwongozo wa Meta kwa wakaguzi na si muhimu wala si kizuizi linganifu kuhusu kujieleza. Maudhui katika kesi hii yanafanana zaidi na maudhui katika uamuzi wa Video Baada ya Shambulio Kanisani Nchini Naijeria, yaliyoonyesha watu waliokufa au waliojeruhiwa kwa karibu, na ishara za wazi sana za vurugu.
Katika kesi hii, kuonyeshwa kwa watoto waliojeruhiwa na waliokufa kunafanya video hiyo kuwa ya kutatiza. Katika hali kama hizi, kuwapatia watumiaji chaguo la iwapo watatazama maudhui ya kutatiza ni uamuzi muhimu na ni hatua inayowiana (tazama pia Video ya Wafungwa wa Kivita wa Armenia).
Bodi imeona kuwa kutojumuisha maudhui yanayoongeza ufahamu wa uwezekano wa ukiukaji wa haki za binadamu na ukiukaji wa sheria kuhusu vita, migogoro au vitendo vya ugaidi kutoka kwenye mapendekezo yanayofikia watu wazima si kizuizi cha lazima au sawia cha uhuru wa kujieleza, kwa kuzingatia kuwa kuna mapendeleo makubwa sana ya umma katika maudhui haya. Skrini za maonyo na uondoaji kutoka kwa mapendekezo hutumika vitofauti, na wakati mwingine zinapaswa kugawanywa, haswa katika hali za mgogoro. Mapendekezo kwenye Instagram yanazalishwa na mifumo otomatiki inayopendekeza maudhui kwa watumiaji kulingana na mapendeleo yaliyobashiriwa ya mtumiaji. Kuondoa maudhui kutoka kwenye mifumo ya mapendekezo kunamaanisha kupunguza ufikiaji ambao maudhui haya yangepata. Bodi inaona kwamba desturi hii inaingilia uhuru wa kujieleza kwa njia zisizo na uwiano kwa vile inatumika kwa maudhui ambayo tayari yanaonekana na watumiaji watu wazima pekee na ambayo yanachapishwa ili kuongeza ufahamu, kushutumu, au kuripoti kuhusu masuala ya mapendeleo ya umma kama vile maendeleo ya mzozo mkali.
Bodi inatambua kuwa majibu ya papo hapo kwa janga yanaweza kuhitaji hatua za kipekee za muda mfupi, na kwamba katika baadhi ya miktadha, ni halali kuweka kipaumbele kwa wasiwasi wa usalama na kuweka vizuizi vya muda na vinavyowiana dhidi ya uhuru wa kujieleza. Baadhi ya hatua hizi zimebainishwa, kwa mfano, katika ahadi za kukabiliana na “maudhui ya ugaidi na vurugu mbaya” zilizowekwa katika Mwito wa Christchurch. Hata hivyo, Bodi imebainisha kuwa Wito wa Christchurch unasisitiza haja ya kujibu maudhui kama haya kwa namna inayolingana na haki za binadamu na uhuru msingi. Bodi inaamini kuwa wasiwasi kuhusu usalama hauna uzito wowote upande wa kuondoa maudhui ya michoro yaliyo na nia ya kutoa uhamasisho kuhusu au kukashifu uwezekano wa uhalifu, uhalifu dhidi ya binadamu au ukiukaji mbaya wa haki za binadamu. Vizuizi kama hivyo vinaweza hata kuzuia maelezo muhimu kwa ajili ya usalama wa watu wanaofuatilia hali katika migogoro hiyo.
Hatua kama vile kutoweka maonyo husaidia kupunguza athari mbaya ambazo huenda hazina uwiano za makosa ya utekelezaji kutokana na hatua za dharura kama vile kupunguza viwango vya uaminifu vya kuondolewa kwa maudhui wakati wa hali za mgogoro. Hata hivyo, hazitoshi kulinda uwezo wa watumiaji kushiriki maudhui yanayotoa uhamasisho kuhusu ukiukaji unaoweza kutokea wa haki za binadamu na ukiukaji wa sheria kuhusu binadamu, na maelezo mengine muhimu katika hali ya mgogoro.
Bodi imeendelea kuangazia mara kwa mara haja ya kubuni mfumo wenye kanuni na wa wazi wa uratibu wa maudhui wakati wa janga na katika maeneo ya mgogoro (Tazama Video ya Kituo cha Polisi nchini Haiti na Shirika la Masuala ya Mawasiliano la Tigray). Ni haswa nyakati za mabadiliko ya haraka ya mgogoro ambapo kampuni kubwa za mitandao ya kijamii zinapaswa kuwekeza rasilimali zinazohitajika ili kuhakikisha kuwa uhuru wa kujieleza haukandamizwi. Katika nyakati kama hizo, vyanzo vya uanahabari huwa vinapitia mashambulizi halisi au mengine, hali inayofanya kuripoti habari na wananchi wa kawaida kwenye mitandao ya kijamii kuwa muhimu.
Bodi pia awali iligundua kuwa katika miktadha ya vita au machafuko ya kisiasa, kutakuwa na maudhui ya michoro na vurugu zaidi yanayonaswa na watumiaji na kushirikiwa kwenye jukwaa kwa madhumuni ya kuongeza uhamasisho au kuchapisha dhuluma (Tazama Video ya Kuogofya ya Sudan). Katika miktadha kama vile ya mgogoro kati ya Israel-Gaza, ambapo kuna idadi ya kutisha ya raia wanaouawa au kujeruhiwa, idadi ya juu ikiwa ni watoto, wakati hali ya kibinadamu ikiendelea kudorora, aina hizi za vighairi ni muhimu sana. Huku ikitambua mchakato unaoendelea wa Meta wa kubuni sera ya Maudhui ya Vurugu na Michoro, Bodi inatarajia Meta iwe tayari kuweka haraka hatua za muda mfupi za kuruhusu aina hii ya maudhui yakiwa na skrini za onyo, na si kuyaondoa kwenye mapendekezo.
Bodi imebaini kuwa hali mjini Gaza kufikia wakati maudhui haya yalichapishwa hayakushirikisha seti sawa ya changamoto kwa Meta kama mashambulizi ya tarehe 7 Oktoba. Mjini Gaza, kumekuwa na ugumu wa kupata maelezo kutoka kwa watu wanaofuatilia hali, huku uwezo wa wanahabari kufikia himaya ukidhibitiwa na muunganisho wa intaneti kukatizwa. Zaidi ya hayo, tofauti na matokeo ya awali ya mashambulizi ya tarehe 7 Oktoba, hali ya Gaza ilivyo katika kesi hii haikuhusisha magaidi kutumia mtandao wa kijamii kutangaza madhila yao. Katika muktadha wa mgogoro wa kivita, kwa kulinganisha, Meta inapaswa kuhakikisha kuwa vitendo vyake havifanyi iwe vigumu zaidi kwa watu kushiriki maudhui yanayotoa malezo yanayotoa uhamasisho kuhusu madhara dhidi ya raia, na yanayoweza kufaa katika kubaini iwapo ukiukaji wa sheria ya kimataifa ya kibinadamu na sheria ya kimataifa ya haki za binadamu umetokea. Swali la iwapo maudhui yalishirikiwa ili kutoa uhamasisho au kukashifu matukio yanayoendelea linapaswa kuwa hatua ya kwanza kwa mkaguzi yeyote anayetathmini maudhui kama hayo, na mifumo otomatiki ya Meta inapaswa kuundwa ili kuzuia uondoaji usio sahihi wa maudhui ambayo yanapaswa kunufaika kutokana na vighairi vinavyotumika.
Kesi hii pia inaonyesha kwamba ukosefu wa uangalizi wa binadamu wa mifumo otomatiki ya uratibu katika muktadha wa mwitikio wa janga unaweza kusababisha kauli iliyo na maslahi ya umma kuondolewa kimakosa. Uamuzi wa awali wa kuondoa maudhui haya pamoja na kukataliwa kwa rufaa ya mtumiaji kulifanywa kiotomatiki kulingana na alama ya kiainishaji, bila ukaguzi wowote wa binadamu. Hali hii, upande mwingine, huenda ulichochewa na mwitikio wa Meta wakati wa janga wa kupungua kiwango cha kuondoa maudhui chini ya sera ya Maudhui ya Vurugu na Michoro kufuatia mashambulizi ya tarehe 7 Oktoba. Hii inamaanisha kuwa hata ikiwa kiainishaji kinatoa alama ya chini zaidi kwa uwezekano wa ukiukaji kuliko inavyohitaji kuwa kwa kawaida, Meta huondoa maudhui hayo.
Ili Meta itumie mifumo otomatiki kwa njia inayolingana na ahadi zake za kulinda haki za binadamu, Bodi inakumbusha Meta kuhusu pendekezo nambari 1 katika kesi ya Katuni Polisi wa Kolombia. Katika kesi hiyo, Bodi ilitoa mwito kwa Meta ihakikishe kwamba maudhui yaliyo na viwango vya juu vya rufaa na viwango vya juu vya rufaa vilivyofaulu yakaguliwe upya ili yaweze kuondolewa kutoka kwa hifadhi zake za Huduma ya Ulinganishaji wa Midia. Katika kuitikia pendekezo hili, Meta iliweka kikundi maalum cha kazi kilichokuwa na jukumu la kuboresha utawala kwenye hifadhi mbalimbali za Huduma ya Ulinganishaji wa Midia (Tazama masasisho ya hivi karibuni ya Meta kuhusu haya hapa). Bodi imebainisha kuwa ni muhimu kwa kikundi hiki kutilia maanani sana matumizi ya Huduma za Ulinganishaji wa Midia katika muktadha wa migogoro ya kivita. Katika kesi ya Dalili za Saratani ya Matiti na Uchi (pendekezo la 3 na 6), Bodi ilipendekeza kuwa Meta ifahamishe watumiaji wakati mifumo otomatiki imetumika kuchukua hatua ya utekelezwaji dhidi ya maudhui yao, na kufichua data kuhusu idadi ya maamuzi ya kuondoa maudhui kiotomatiki kulingana na Viwango vya Jumuiya na uwiano wa maamuzi hayo ambayo baadaye hubatilishwa kufuatia ukaguzi wa binadamu. Hii ni muhimu haswa wakati viwango vya uaminifu vya maudhui ambayo yana uwezekano mkubwa wa ukiukaji vimeripotiwa kuwa vimepunguzwa pakubwa. Bodi inahimiza Meta kufanya hatua zaidi katika utekelezaji wa pendekezo la 6 na kushiriki ushahidi wa utekelezaji na Bodi kwa ajili ya pendekezo la 3.
Vizuizi dhidi ya uhuru wa kujieleza lazima viwe visivyobagua, ikiwa ni pamoja na kwa msingi wa utaifa, kabila, dini au imani, au maoni ya kisiasa au mengine (Kifungu cha 2, aya ya 1, na Kifungu cha 26, ICCPR). Utekelezaji wa Viwango vya Jumuiya kwa ubaguzi unahujumu kigezo cha kimsingi cha uhuru wa kujieleza. Katika kesi ya Chapisho Lililoshirikiwa la Al Jazeera, Bodi iliibua wasiwasi mkubwa kwamba makosa katika uratibu wa maudhui unaofanya na Meta katika Israeli na Himaya Zinazokaliwa za Upalestina huenda zimesambazwa kwa njia isiyo ya sawa, na kutoa mwito wa uchunguzi huru kufanywa (Uamuzi kuhusu Chapisho Lililoshirikiwa la Al Jazeera, pendekezo nambari 3). Shughuli ya Wajibu wa Kijamii (BSR) Tathmini ya Athari ya Haki za Binadamu, ambayo Meta ilianzisha ili kuitikia pendekezo hilo, ilitambua “matukio kadhaa ya mapendeleo ambayo hayakunuiwa ambapo sera na desturi za Meta, pamoja na hali pana za nje, husababisha athari tofauti za haki za binadamu kwa watumiaji wa Upalestina na wanaozungumza Kiarabu.” Bodi inahimiza Meta kufanikisha ahadi zake katika kuitikia ripoti ya BSR.
Hatimaye, Meta ina wajibu wa kuhifadhi ushahidi wa uwezekano wa ukiukaji wa haki za binadamu na ukiukaji wa sheria za kimataifa za binadamu, kama inavyopendekezwa pia katika ripoti ya BSR (pendekezo la 21) na kutetewa na vikundi vya kiraia. Hata wakati maudhui yanapoondolewa kwenye majukwaa ya Meta, ni muhimu kuhifadhi ushahidi kama huo kwa ajili ya maslahi ya uwajibikaji wa siku zijazo (Tazama Video ya Kuogofya ya Sudan na Video ya Wafungwa wa Kivita wa Armenia). Ingawa Meta ilieleza kuwa inahifadhi maudhui yote ambayo yanakiuka Viwango vya Jumuiya yake kwa muda wa mwaka mmoja, Bodi inahimiza kwamba maudhui yanayohusiana haswa na uhalifu wa kivita unaoweza kutokea, uhalifu dhidi ya binadamu, na ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu yatambuliwe na kuhifadhiwa kwa njia ya kudumu na inayoweza kufikiwa zaidi kwa madhumuni ya uwajibikaji wa muda mrefu. Bodi inabaini kuwa Meta imekubali kutekeleza mapendekezo nambari 1 katika kesi ya Video ya Wafungwa wa Kivita wa Armenia Hii ilitaka Meta iunde itifaki ya kuhifadhi na, inapofaa, kushiriki na mamlaka husika, taarifa za kusaidia katika uchunguzi na michakato ya kisheria ili kurekebisha au kushtaki uhalifu wa ukatili au ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu. Meta imefahamisha Bodi kuwa iko katika hatua za mwisho za kuandaa "mbinu thabiti ya kuhifadhi ushahidi unaoweza kuwa wa uhalifu wa kikatili na ukiukaji mkubwa wa sheria za kimataifa za haki za binadamu” na inatarajia kuipa Bodi taarifa fupi kuhusu mbinu yake hivi karibuni. Bodi inatarajia Meta kutekeleza mapendekezo yaliyo hapa juu kikamilifu.
*Kidokezo cha Utaratibu:
Maamuzi ya haraka ya Bodi ya Usimamizi yanatayarishwa na majopo ya wanachama watano na hayategemei idhini ya wanabodi wengi. Maamuzi ya Bodi hayawakilishi maoni ya kibinafsi ya wanachama wote.
Voltar para Decisões de Casos e Pareceres Consultivos sobre Políticas