Overturned
Mwanamke wa Iran Akabiliwa Mtaani
March 7, 2024
Bodi ya Usimamizi imebatilisha uamuzi wa kwanza wa Meta wa kuondoa video inayoonyesha mwanaume akimkabili mwanamke katika barabara za Irani kwa kuwa mwanamke huyo hakuvaa hijabu.
Muhtasari
Bodi ya Usimamizi imebatilisha uamuzi wa kwanza wa Meta wa kuondoa video inayoonyesha mwanaume akimkabili mwanamke katika barabara za Irani kwa kuwa mwanamke huyo hakuvaa hijabu. Chapisho hilo halikukiuka kanuni za Vurugu na Uchochezi kwa sababu lilikuwa na kauli ya kimafumbo, badala ya halisi, na si tishio la kusadikika la vurugu. Lilishirikiwa wakati wa mzozo, na kuongeza uonevu na vurugu dhidi ya watu waliokuwa wakiandamana, ufikiaji wa mitandao ya kijamii nchini Irani ni muhimu huku intaneti ikiwakilisha uwanja mpya wa mapambano katika juhudi za kupigania haki za wanawake. Kwa kuwa Instagram ni mojawapo ya majukwaa kadhaa yaliyosalia ambayo hayajapigwa marufuku nchini humo, nafasi yake katika vuguvugu la kupiga utawala la “Wanawake, Maisha, Uhuru” haina kipimo, licha ya juhudi za utawala kuweka wanawake uwoga na kuwanyamazisha mtandaoni. Bodi inahitimisha kwamba juhudi za Meta za kuhakikisha heshima kwa uhuru wa kujieleza na kukusanyika katika muktadha wa uonevu wa kimfumo wa serikali hazijatosha na inapendekeza mabadiliko yafanywe katika Itifaki ya Sera ya Janga ya kampuni hiyo.
Kuhusu Kesi
Mnamo Julai 2023, mtumiaji alichapisha video kwenye Instagram ambapo mwanaume fulani alimkabili mwanamke hadharani kwa kutovaa hijabu. Katika video hiyo, iliyo katika Kiajemi na manukuu ya Kiingereza, mwanamke huyo anajibu kwa kusema kuwa anasimama kupigania haki zake. Manukuu yanayoambatana yanaeleza uungaji mkono wa mwanamke huyo na wanawake wa Irani wanaopinga utawala. Sehemu ya manukuu, ambayo pia yanasuta utawala, inajumuisha kauli inayotafsiriwa kama, “haipo mbali kukufanya kuwa vipande,” kulingana na Meta.
Sheria ya adhabu ya Irani iliwaadhibu wanawake waliojitokeza hadharani bila “hijabu inayofaa” kwa kifungo gerezani, kutozwa faini au kuchapwa viboko. Mnamo Septemba 2023, utawala wa Irani uliidhinisha Sheria mpya ya Hijabu na Ubikira ambayo kwa mujibu wake, wanawake wangekabiliwa na kifungo cha hadi miaka 10 gerezani ikiwa wangeendelea kukaidi kanuni za lazima za hijabu. Manukuu kwenye chapisho hili yanaifanya kuwa wazi kuwa mwanamke aliye kwenye video tayari amekamatwa.
Kwanza lilialamishwa na mifumo otomatiki ya Meta kwa uwezekano wa kukiuka Miongozo ya Jumuiya ya Instagram, chapisho hilo lilitumwa kwa wakaguzi binadamu. Ingawa wakaguzi kadhaa walitathmini maudhui hayo chini ya sera ya Vurugu na Uchochezi ya Meta, hawakufanya uamuzi sawa, hali ambayo, pamoja na hitilafu ya kiufundi, ilimaanishwa kuwa chapisho hilo lingesalia kwenye jukwaa. Mtumiaji kisha aliripoti chapisho hilo, hali iliyosababisha awamu ya ziada ya ukaguzi, mara hii na timu ya kikanda ya Meta pamoja na wataalamu wa lugha. Katika hatua hii, ilibainika kwamba chapisho hilo lilikiuka sera ya Vurugu na Uchochezi na liliondolewa kwenye Instagram. Mtumiaji ambaye alichapisha maudhui hayo kisha alikata rufaa kwa Bodi. Meta ilikariri kuwa uamuzi wake wa kuondoa maudhui hayo ulikuwa sahihi hadi Bodi ilipoteua kesi hii, katika hatua hii, kampuni hiyo ilibatilisha uamuzi wake, na ikarejesha chapisho hilo.
Matokeo Muhimu
Bodi imepata kuwa chapisho hilo halikiuki Viwango vya Jumuiya kuhusu Vurugu na Uchochezi kwa sababu lina kauli ya kimatamathali, badala ya sisisi, na si tishio la kusadikika la vurugu linaloweza kuchochea madhara ya nje ya mtandao. Ingawa awali Meta iliondoa chapisho hilo, mojawapo ya sababu zake ikiwa kuwa ilitathmini kauli, “haipo mbali na kukufanya kuwa vipande,” kama kauli ya nia ya kusababisha vurugu ya ubaya wa juu – ikilenga mwanaume aliye kwenye video – haipaswi kutafsiriwa kwa njia sisisi. Kutokana na muktadha wa maandamano yaliyokithiri nchini Irani, na manukuu na video kwa jumla, kauli hii ni ya kimajazi na inaelezea hasira na kufadhaishwa na utawala. Wataalamu wa isimu walioshauriana na Bodi walibaini tafsiri tofauti kidogo ya kauli (“tutakurarua katika vipande hivi karibuni”), wakieleza kwamba inaelezea hasira, kutamaushwa na chuki dhidi ya utawala. Badala ya kuchochea madhara dhidi ya utawala, chapisho hili lilikuwa na uwezo wa kusababisha vurugu za kulipiza kisasi ambacho kingetekelezwa na utawala.
Ingawa mtazamo wa sera ya Meta unapendekeza kuwa “lugha” na “muktadha” unaweza kuzingatiwa wakati wa kutathmini “tishio la kusadikika,” mwongozo wa ndani wa Meta kwa waratibu hauwezeshi desturi hii. Waratibu wameagizwa kutambua vigezo mahususi (tishio na mlengwa) na ikiwa vigezo hivyo vimetimizwa, kuondoa maudhui. Awali Bodi ilibaini wasiwasi wake kuhusu ukosefu huu wa uwiano katika kesi ya Kauli Mbiu ya Maandamano ya Irani, ambapo inapendekeza kwamba Meta itoe mwongozo wenye hali zote kuhusu jinsi ya kuzingatia muktadha, kuelekeza waratibu kuacha uondoaji chaguo-msingi wa “lugha ya balagha” inayoonyesha kutokubaliana. Inatia wasiwasi kwamba bado kuna nafasi ya utekelezwaji usio sawa wa kauli za tamathali, katika muktadha kama wa Irani. Zaidi ya hayo, kwa sababu usahihi wa mifumo otomatiki unaathiriwa na ubora wa data ya mafunzo inayotolewa na binadamu, kuna uwezekano kwamba kosa la uondoaji wa kauli za tamathali likaongezeka.
Chapisho hili pia lilizingatiwa chini ya Viwango vya Jumuiya kuhusu Kupanga Madhara na Kuendeleza Uhalifu kwa sababu kuna sheria inayopiga marufuku “maudhui yanayoweka wanawake wasiovaa shela katika hatari ya kufichukua picha zao bila shela za kujifunika kinyume na matakwa au idhini yao.” Mkondo huo wa sera umebadilishwa ili kupiga marufuku: “Kufichua [kumfichua mwanamke] kufichua utambulisho wa mtu na kumweka katika hatari ya madhara.” Kuhusiana na hili, Bodi inakubaliana na Meta kwamba maudhui hayo “hayamfichui” mwanamke aliye kwenye video na hatari ya madhara ilikuwa imezuiwa kwa sababu utambulisho wake ulifahamika kwa wengi na tayari alikuwa ameshakamatwa. Hakika, chapisho hilo lilishirikiwa ili kutoa habari kuhusu kukamatwa kwake na lingesaidia kushinikiza mamlaka kumwachilia huru.
Kwa kuwa Irani imebainishwa kama nchi iliyo hatarini chini ya sera za janga za Meta, ikiwa ni pamoja na Itifaki ya Sera ya Janga, kampuni hiyo inaweza kutekeleza mabadiliko ya muda ya sera (“wenzo”) ili kushughulikia hali mahususi. Ingawa Bodi inatambua juhudi za Meta kuhusiana na Irani, juhudi hizi hazijatosha katika kuhakikisha uhuru wa watu kujieleza na kukutana unaheshimiwa katika mazingira ya uonevu wa kimfumo.
Uamuzi wa Bodi ya Usimamizi
Bodi ya Usimamizi imebatilisha uamuzi wa awali wa Meta wa kuondoa chapisho hilo.
Bodi inapendekeza kwamba Meta:
- Iongeze wenzo kwenye Itifaki ya Sera ya Janga ili kufanya iwe wazi kwamba kauli za kitamathali (yaani si sisisi) ambazo hazinuiwi na hazina uwezo wa kuchochea vurugu, hazikiuki sera ya Vurugu na Uchochezi inayopiga marufuku vurugu katika muktadha husika. Hii inapaswa kujumuisha kuunda vigezo kwa waratibu wa kiwango kuhusu jinsi ya kutambua kauli kama hizi katika muktadha husika.
*Mihtasari ya kesi hutoa maelezo mafupi ya kesi hizi na haina thamani ya kurejelewa katika kesi za baadaye.
Uamuzi Kamili wa Kesi
1. Muhtasari wa Uamuzi
Bodi ya Usimamizi imebatilisha uamuzi wa kwanza wa Meta wa kuondoa video ambayo inaonyesha mwanaume akimkabili mwanamke katika barabara za Irani kwa kuwa mwanamke huyo hakuvaa hijabu. Meta iliondoa chapisho hilo kwenye Instagram kwa sababu ya mstari ufuatao wa manukuu – “haipo mbali sana kukufanya uwe vipande” – kauli ambayo kampuni ilitafsiri kama tishio, linalomlenga mwanaume kwenye video ambaye alimkabili mwanamke ambaye alivaa hijabu. Bodi imepata kuwa chapisho hilo halikukiuka sera ya Vurugu na Uchochezi kwa sababu kauli husika ni ya kitamathali, badala ya sisisi na kutokana na muktadha huo, chapisho hili si tishio la kusadikika la vurugu. Baada ya Bodi kuchagua kesi hii, Meta awali ilidumisha uamuzi wake wa kuondoa chapisho - hata hivyo, kabla ya kutuma utaratibu wake kwa Bodi, Meta ilibaini kuwa uamuzi wake wa kwanza wa kuondoa maudhui ulifanywa kimakosa na ilirejesha chapisho hilo kwenye jukwaa. Bodi inahitimisha kwamba juhudi za Meta za kuhakikisha heshima kwa uhuru wa kujieleza na kukusanyika katika muktadha wa uonevu wa kimfumo wa serikali hazijatosha na inapendekeza mabadiliko yafanywe katika Itifaki ya Sera ya Janga ya kampuni.
2. Maelezo na Historia ya Kesi
Mnamo Julai 2023, mtumiaji wa Instagram alichapisha video kwa Kiajemi na manukuu ya Kiingereza yanayoonyesha mwanaume akimkabili mwanamke hadharani kwa kutovaa hijabu, huku mwanamke huyo akijibu kwamba anatetea haki zake. Mwanaume huyo hawezi kutambuliwa kwenye video ilhali mwanamke huyo hapatikani. Video inaonekana kuwa rekodi iliyochapishwa tena ambayo mwanzo ilishirikiwa na mtu anayeegemea au kuunga mkono utawala wa Irani. Video hiyo ina manukuu, pia kwa Kiajemi, inayoonyesha uungaji mkono wa mwanamke huyo na kwa wanawake wa Irani wanaopigania utawala na kusuta utawala na wafuasi wake. Manukuu hayo yalijumuisha kauli inayotafsiriwa na Meta kama, “haipo mbali na kukufanya uwe vipande” na yalisema kwamba mwanamke huyo alikamatwa kufuatia tukio hilo. Chapisho hilo lilikuwa limetazamwa mara 47,000, likapendwa mara 2,000, maoni 100 na kushirikiwa mara 50.
Maudhui haya yalialamishwa kwanza na kiainishaji otomatiki, algoriti ambayo Meta hutumia kutambua uwezekano wa ukiukaji wa sera zake, kuwa yalikuwa na uwezekano wa kukiuka Miongozo ya Jumuiya ya Instagram na yakatumwa ili yafanyiwe ukaguzi wa binadamu. Wakaguzi wengi walitathmini maudhui hayo, lakini kwa sababu ya hitilafu ya kiufundi na kwa sababu wakaguzi hawakufanya uamuzi sawa kuhusu iwapo chapisho hilo lilikuwa la ukiukaji wa sera ya Vurugu na Uchochezi, awali hayakuondolewa. Mtumiaji kisha aliripoti maudhui hayo, katika kujibu kile kiainishaji otomatiki kilibaini tena kuwa maudhui hayo yalikuwa na uwezekano wa kukiuka sera za Meta na kuyatuma kwa ukaguzi wa ziada. Maudhui hayo yaliripotiwa na mtumiaji mmoja na yaliripotiwa tu mara moja. Kufuatia kiwango hiki cha ziada cha ukaguzi na timu ya Meta pamoja na wataalamu wa kikanda na wa lugha, Meta iliondoa chapisho hilo kutoka kwa Instagram chini ya sera yake ya Vurugu na Uchochezi. Uamuzi wa Meta wa kuondoa chapisho hilo ulitokana na mstari ufuatao kwenye manukuu: “haipo mbali na kukufanya kuwa vipande.” Kampuni hiyo ilitafsiri mstari huu kama tishio, linamlenga mwanaume aliye kwenye video ambaye alimkabili mwanamke kwa kutovaa hijabu. Mtumiaji aliyeunda chapisho hilo alikata rufaa dhidi ya uamuzi wa kuondoa chapisho hilo kwa Meta. Mkaguzi aliunga mkono uamuzi wa kuliondoa.
Mtumiaji ambaye alichapisha maudhui hayo kisha alikata rufaa dhidi ya uondoaji huo kwa Bodi. Bodi ilipotambua kesi hii kwa ukaguzi wa kisheria, Meta ilidumisha uamuzi wake wa kuondoa maudhui. Katika hatua ya ukaguzi, Meta pia ilizingatia Viwango vya Jumuiya kuhusu Kupanga Madhara na Kuendeleza Uhalifu, ambavyo vinapiga marufuku “kushambulia” mwanamke ambaye hajajifunika wakati kufanya hivyo kunamfanya mwanamke huyo kuwa hatarini kupata madhara. Kufikia wakati ambapo maudhui hayo yalichapishwa, mwanamke huyo tayari alikuwa amekamatwa na utawala. Baada ya Bodi kuchagua kesi hii, kampuni hiyo ilibadilisha uamuzi wake na ikarejesha maudhui hayo kulingana na mchango wa ziada kutoka kwa timu ya kikanda na uamuzi wa Bodi katika kesi ya Mwito wa Maandamano ya Wanawake nchini Kuba.
Kama Bodi iliyobaini katika uamuzi wake wa Kauli Mbiu ya Maandamano ya Irani, watu nchini Irani wamekuwa wakiandamana dhidi ya serikali na kwa kupigania haki za kiraia na kisiasa pamoja na usawa wa kijinsia, tangu angalau mageuzi ya 1979. Mnamo 2023, Tuzo za Amani za Nobel zilitolewa kwa Narges Mohammadi, mpiganiaji wa haki za binadamu aliyekuwa mfungwa, kwa “zaidi ya miaka 20 ya kupigania haki za wanawake [hali ambayo] imemfanya kuwa ishara ya uhuru na viwango katika mapambano dhidi ya mfumo wa utawala wa kidini nchini Irani.” Sheria ya adhabu ya Irani huwaadhibu wanawake wanaojitokeza hadharani bila “hijabu inayofaa” kwa kifungo gerezani, kutozwa faini au kuchapwa viboko. Wanawake nchini Irani pia wamepigwa marufuku kusomea baadhi ya taaluma na kutembelea maeneo mengi ya umma, na watu hawaruhusiwi kucheza dansi na watu wa jinsia tofauti, miongoni mwa mambo mengine. Wanaume wanachukuliwa kuwa wakuu wa kaya na wanawake wanahitaji ruhusa ya baba au mume wao ili kufanya kazi, kuoa au kusafiri. Ushahidi wa mahakama wa mwanamke unazingatiwa kuwa nusu ya uzito wa ushahidi wa mwanaume, hali inayowekea kizuizi uwezo wa wanawake kupata haki.
Baada ya mamlaka za Irani kuongeza na kupanua utekelezaji wa hatua ya kulazimisha mavazi ya hijabu mwaka 2022, wanawake wamepitia hali ya kuongezeka kwa uchunguzi, mara nyingi ikisababisha unyanyasaji wa maongezi na kimwili na kukamatwa. Mnamo Septemba 2022, mwanadada mwenye umri wa miaka 22 anayefahamika kama Jina Mahsa Amini alikufa akiwa gerezani siku tatu baada ya kukamatwa kwa tuhuma za kukosa kutii sheria za nchi kuhusu kuvaa “hijabu inayofaa.” Kifo chake kilichochea hasira kote nchini na misururu ya maandamano kote nchini humo, na vuguvugu la kupinga serikali ambalo linafahamika kama: “Zan, Zendegi, Azadi” (“Wanawake, Maisha, Uhuru”). Hali hii imefanya mamlaka kuwachukulia hatua kali, huku zaidi ya watu 500 wakithibitishwa kufariki kufikia mwisho wa 2022, na idadi inayokadiriwa kuwa watu 14,000 kukamatwa, hii ikiwa ni pamoja na waandamanaji, wanahabari, mawakili, wanaharakati, wasanii na wanariadha walioonyesha kuunga mkono vuguvugu hilo.
Mnamo Septemba 2023, bunge la Irani liliidhinisha “sheria mpya ya Hijabu na Ubikira” ambayo kwa mujibu wake, wanawake wangekabiliwa na kifungo cha hadi miaka 10 gerezani ikiwa wangeendelea kukaidi kanuni za lazima za hijabu za nchi hiyo. Biashara zinazowahudumia wanawake wasiovaa hijabu pia zingewekewa vikwazo na kujiweka katika hatari ya kufungwa.
Mitandao ya Kijamii imekuwa nguzo muhimu katika harakati za maandamano za wanawake nchini Irani, ikichukua nafasi muhimu katika kupanga maandamano na kutangaza taarifa muhimu (angalia maoni ya umma PC 21007, PC-21011), na katika kuweka pamoja makala na kuhifadhi hadharani ushahidi kuhusu dhuluma na ukiukaji wa haki za binadamu (PC-21008, kiambatisho).
Hata hivyo, kampeni za mtandaoni pia zinawaweka wanawake katika hatari ya maonevu zaidi na utawala, ikiwa ni pamoja na vitisho, kampeni za ushushaji hadhi, kukamatwa na kufungwa jela. Wataalamu ambao Bodi ilishauriana nao walibaini mtandao mrefu wa mashirika yanayohusiana na Islamic Revolutionary Guard Corps na serikali ya Irani inayoendesha shughuli zake kwenye Instagram na Telegram, huku Telegram ikitumika sana kuwalenga moja kwa moja na kukashifu waaandamanaji na wapinzani.
Maoni kadhaa ya umma yaliyotumwa kwa Bodi pia yaliangazia mbinu ya utawala ya kuripoti maudhui ya visa vingi vya maandamano kwenye Instagram kwa kutumia mfumo wa mtumiaji kuripoti ili “kushinikiza kampuni za mitandao ya kijamii kuondoa maudhui yanayohusiana na upinzani au kuzuia kuonekana kwa maudhui yao” (angalia maoni ya umma PC-21011, PC-21009). Pia kumekuwa na ripoti za maafisa wa ujasusi wa Irani kuwapatia waratibu wa maudhui pesa ili waondoe maudhui yanayoshirikiwa na watu wanaosuta utawala.
Mnamo Februari 2023, Mjumbe Maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu Irani aliripoti wasiwasi kuhusu kuendelea kwa uonevu dhidi ya wanaharakati wa haki kijamii, watetezi wa haki za binadamu, wanaharakati wa haki za kina mama, mawakili na wanahabari, wakati mamlaka zilikuwa zikifunga njia za kuonyesha upinzani, ikiwa ni pamoja na kuingia pakubwa matumizi ya mtandao na udhibiti wa mitandao ya kijamii.
3. Bodi ya Usimamizi na Upeo
Bodi ina mamlaka ya kukagua uamuzi wa Meta kufuatia rufaa kutoka kwa mtu ambaye maudhui yake yaliondolewa (Kifungu cha 2 cha Mkataba, Sehemu ya 1; Sheria ndogo za Kifungu cha 3, Sehemu ya 1).
Bodi inaweza kudumisha au kubatilisha uamuzi wa Meta (Kifungu cha 3, Sehemu ya 5 ya Mkataba), na kampuni itafuata uamuzi huu (Kifungu cha 4 cha Mkataba). Meta pia lazima itathmini uwezekano wa kutekeleza uamuzi wake kuhusiana na maudhui yanayofanana yaliyo katika muktadha tofauti (Kifungu cha 4 cha Mkataba). Uamuzi wa Facebook unaweza kujumuisha mapendekezo yasiyo ya kufunga ambayo Meta lazima iyajibu (Kifungu cha 3 cha Mkataba, Sehemu ya 4); Kifungu cha 4). Wakati Meta inajitolea kushughulikia mapendekezo, Bodi hufuatilia utekelezaji wake.
Bodi inapochagua kesi kama hii, ambapo Meta, baadaye inakubali kwamba ilifanya makosa, Bodi hukagua uamuzi wa kwanza wa kuongeza ufahamu wa mchakato wa udhibiti wa maudhui na kutoa mapendekezo ili kupunguza makosa na kuongeza usawa kwa watu wanaotumia Facebook na Instagram.
4. Vyanzo vya Mamlaka na Mwongozo
Viwango vifuatavyo na kesi za awali zilikuwa msingi wa uchanganuzi wa Bodi katika kesi hii:
I. Maamuzi ya Bodi ya Usimamizi
Maamuzi muhimu zaidi ya awali ya Bodi ya Usimamizi yanajumuisha:
- Mwito wa Maandamano ya Wanawake nchini Kuba
- Kauli za Kimafumbo Dhidi ya Rais wa Peru
- Kauli Mbiu ya Maandamano ya Iran
- Kutengwa kwa Öcalan
- Dalili za Saratani ya Matiti na Picha ya Uchi
II. Sera za maudhui za Meta
Uchanganuzi wa Bodi ulitokana na ahadi ya Meta ya kulinda sauti, ambayo kampuni hiyo inaeleza kuwa ni “muhimu,” na maadili yake ya usalama, faragha na heshima.
Miongozo ya Jumuiya ya Instagram
Miongozo ya Jumuiya ya Instagram inasema kwamba kampuni hiyo “itaondoa maudhui yaliyo na vitisho vya kusadikika” na kuunganisha Viwango vya Jumuiya kuhusu Vurugu na Uchochezi. Miongozo ya Jumuiya haiunganishwi moja kwa moja na Viwango vya Jumuiya kuhusu Kupanga Madhara na Kuendeleza Uhalifu. Ripoti ya Utekelezaji wa Viwango vya Jumuiya ya Meta ya Q1 2023 inasema kuwa “Facebook na Instagram hushiriki Sera za Maudhui. Hii inamaanisha kwamba ikiwa maudhui yanazingatiwa kuwa ya ukiukaji kwenye Facebook, pia yanazingatiwa kuwa ya ukiukaji kwenye Instagram.”
Maudhui hayo yaliondolewa chini ya sera ya Vurugu na Uchochezi. Baada ya Bodi kuchagua kesi hii, Meta ilichanganua maudhui hayo chini ya sera yake dhidi ya Kupanga Madhara na Kuendeleza Uhalifu.
Kiwango cha Jumuiya kuhusu Vurugu na Uchochezi
Kulingana na mtazamo wa sera, Viwango vya Jumuiya kuhusu Vurugu na Uchochezi vinanuia “kuzuia uwezekano wa vurugu ya nje ya mtandao ambayo inaweza kuwa inahusiana na maudhui” yanayoonekana kwenye majukwaa ya Meta. Wakati huohuo, Meta inatambua kwamba “watu kwa kawaida wanaonyesha madharau au kutokubaliana kwa kutoa vitisho au kuita vurugu katika njia za kimzaha zisizo rasmi.” Kwa hivyo Meta huondoa maudhui wakati kampuni hiyo inaamini maudhui yana “vitisho vya vurugu zinazoweza kusababisha kifo,” ikiwa ni pamoja na maudhui yanayolenga yeyote kwa “taarifa za nia” ili kufanya “vurugu za ubaya wa juu.” Inasema kwamba inazingatia muktadha wa kauli inapotathmini iwapo tishio fulani ni la kusadikika, ambayo inaweza kuwa taarifa yoyote ya ziada kama vile “uonekanaji wa umma na mlengwa kuwa hatarini.”
Sehemu ya “usichapishe” ya sera inapiga marufuku “vitisho vya vurugu zinazoweza kusababisha kifo (na namna nyingine za vurugu za ubaya wa juu).” Neno “tishio” linajumuisha “taarifa za nia” ya kutekeleza vurugu za ubaya wa juu.
Viwango vya Jumuiya kuhusu Kupanga Madhara na Kuendeleza Uhalifu
Kulingana na mtazamo wa sera, Viwango vya Jumuiya kuhusu Kupanga Madhara na Kuendeleza Uhalifu vinalenga “kukatiza uhalifu wa nje ya mtandao na tabia ya uigaji” kwa kuwakataza watu dhidi ya “kufadhili, kupanga, kuendeleza au kukubali shughuli fulani za uhalifu au za madhara zinazowalenga watu, biashara, mali au wanyama.” Hii ni pamoja na “ufichuzi wa utambulisho,” ambayo Meta inafafanua kuwa maudhui yanayofichua utambulisho au maeneo yanayohusishwa na mtu yeyote ambaye anatuhumiwa kuwa, miongoni mwa mambo mengine, “mwanachama wa kikundi cha hatari ya ufichuzi wa utambulisho.” Mkondo huu wa sera inatekelezwa na waratibu katika kiwango kuhusiana na makundi fulani mahususi. Baada ya kupendekezwa kwa Bodi, pamoja na muktadha wa ziada, sera ya Meta kufikia wakati maudhui hayo yalichapishwa ilisema kwamba inaweza pia kuondoa: “maudhui yanawaweka wanawake ambao hawajajifunika katika hatari kwa kufichua picha zao wakiwa hawana hijabu kinyume na matakwa au bila idhini yao.” Lugha hii sasa imehaririwa ili kupiga marufuku: “kufichua utambulisho wa [wanawake wasiojifunika]: kuweka peupe utambulisho wa mtu na kumweka katika hatari ya madhara.”
III. Wajibu wa Meta wa Haki za Binadamu
Kanuni za Mwongozo wa Umoja wa Mataifa juu ya Biashara na Haki za Binadamu (UNGP), zilizoidhinishwa na Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa mnamo 2011, zina mfumo wa hiari wa majukumu ya haki za binadamu ya biashara za kibinafsi. Sera ya Kishirika ya Haki za Binadamu ya Meta, iliyotangazwa tarehe 16 Machi 2021, ilisisitiza ahadi ya kampuni hiyo kuheshimu haki kama ilivyoakisiwa kwenye UNGP.
Viwango vifuatavyo vya kimataifa vinaweza kuwa muhimu katika uchambuzi wa Bodi wa wajibu wa haki za binadamu wa Meta katika kesi hii:
- Haki ya uhuru wa kujieleza: Kifungu cha 19, Mkataba wa Kimataifa kuhusu Haki za Kiraia na Siasa ( ICCPR), Maoni ya Jumla Nambari. 34, Kamati ya Haki za Binadamu, 2011; Mjumbe Maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu uhuru wa maoni na kujieleza, anaripoti: A/HRC/38/35 (2018) na A/74/486 (2019); na Mpango wa Hatua wa Rabat, ripoti ya Tume ya Kamishna Mkuu wa Umoja wa Mataifa wa Haki za Binadamu: A/HRC/22/17/Add.4 (2013).
- Haki ya uhuru wa kufanya mkutano kwa amani: Kifungu cha 21, ICCPR: Maoni ya Jumla Nambari 37, Kamati ya Haki za Binadamu, 2020.
- Haki ya kuishi: Kifungu cha 6, ICCPR.
- Haki ya uhuru na usalama wa mtu: Kifungu cha 9, ICCPR;
- Haki ya kutobaguliwa: Vifungu vya 2(1), 3 na 26, ICCPR; Kifungu cha 1 na cha 7 (kutobagua katika kushiriki katika maisha ya kisiasa na ya umma ya nchi), Mkutano kuhusu Uondoaji wa Namna Zote za Ubaguzi dhidi ya Wanawake (CEDAW). Tazama Azimio kuhusu Watetezi wa Haki za Binadamu, Kifungu cha 8, haki ya ufanisi katika ufikiaji, kwa msingi wa kutobaguliwa, ili kushiriki katika uendeshaji wa masuala ya umma.
- Haki ya faragha: Kifungu cha 17, ICCPR.
5. Mawasilisho ya Mtumiaji
Mtumiaji ambaye alichapisha maudhui hayo alikata rufaa dhidi ya uondoaji huo kwa Bodi. Katika taarifa yake, mtumiaji huyo alieleza kuwa chapisho hilo lilionyesha mwakilishi wa serikali ya Iran akikabili mwanamke kwa kutovaa hijabu. Mtumiaji alitaja kwamba video hiyo inaonyesha ujasiri wa mwanamke wa Iran akitetea haki zake. Mtumiaji huyo alitaja kwamba wengine walikuwa wameshiriki video inayofanana na hiyo kwenye mitandao ya kijamii na kwamba maudhui hayo hakuwa yenye madhara wala hatari na hayakukiuka sera yoyote ya Instagram.
6. Mawasilisho ya Meta
Kiwango cha Jumuiya kuhusu Vurugu na Uchochezi
Meta ilifahamisha Bodi kwamba uamuzi wake wa awali wa kuondoa maudhui katika kesi hii ulitokana na sera ya Vurugu na Uchochezi. Ilieleza kwamba uamuzi wake ulitokana na sehemu ya manukuu ya chapisho hilo, ambayo kampuni hiyo ilitafsiri kama: “haipo mbali kukufanya kuwa vipande.” Kampuni hiyo ilitafsiri mstari huu kama uliomlenga mwanaume aliye kwenye video ambaye alimkabili mwanamke kwa kutovaa hijabu. Timu yake ya kikanda ilibaini kwamba kauli “kufanya kuwa vipande” ilikuwa ni tishio la madhara ya kimwili katika muktadha wa Iran. Kutokana na ufasiri huo, Meta awali ilidumisha uamuzi wa kuondoa maudhui hayo chini ya sera yake ya Vurugu na Uchochezi.
Ingawa Meta ilidumisha uamuzi wake wa kuondoa maudhui wakati Bodi ilitambua kesi hii kwa mara ya kwanza ili kufanyiwa ukaguzi wa kisheria, baadaye ilibadilisha uamuzi wake baada ya Bodi kuchagua kesi hii na ikarejesha maudhui hayo kulingana na mchango wa ziada kutoka kwa timu ya kikanda. Kulingana na mchango huo, Meta ilihitimisha kwamba ufasiri unaowezekana wa lugha katika manukuu hayo ulikuwa unarejelea kuondoa utawala wa Iran au wale waliokuwa wakiunga mkono kanuni ya lazima ya kuvaa hijabu, badala ya tishio la moja kwa moja kwa mwanaume aliye kwenye video hiyo.
Katika ukaguzi huu wa mwisho, Meta ilihitimisha kwamba maudhui hayo yalinuia kutoa uhamasisho na kuvutia makini katika dhuluma zinazofanywa dhidi ya wanawake, kama vile mwanamke anayekabiliwa na mwanaume katika video kwa kutovaa hijabu. Mtumiaji anarejelea nguvu ya wanawake wa Iran na kusuta “ukatili,” akirejelea ama mwanaume anayerekodi video au utawala mzima na kutoa uhamasisho kuhusu kukamatwa kwa mwanamke kwenye video husika. Meta ilieleza kwamba lugha yenye uwezekano wa kutishia unapaswa kusomwa na kueleweka katika muktadha huu kwa jumla. Aina hii ya kutoa uhamasisho, Meta ilibaini kwenye mtazamo wake, ikitaja uamuzi wa Bodi katika kesi ya Kauli Mbiu ya Maandamano ya Iran, ni muhimu hasa nchini Iran ambapo njia za kujieleza huru ni finyu.
Meta pia ilifahamisha Bodi kwamba baada ya utafiti zaidi, timu za kikanda zilipendekeza kwamba ufasiri ufaao zaidi wa lugha “haipo mbali na kukufanya kuwa vipande” haukuwa tishio la kweli, badala yake kauli ya kisiasa inayolenga ama utawala kwa jumla au watu wanaounga mkono masharti ya kuvaa hijabu kwa lazima kwa ujumla zaidi. Ingawa “kufanya kuwa vipande” kwa jumla kunarejelea kuuwa mtu kwa kukata mwili wake vipande, hapa inaweza kueleweka kama kusambaratisha utawala (sawa na lugha ya kimafumbo inayotumika katika uamuzi wa muhtasari katika Kauli ya Kimafumbo Dhidi ya Rais wa Peruu).
Meta ilifahamisha Bodi kwamba kigezo kingine kilichosababisha kampuni hatimaye kurejesha maudhui kilikuwa ni uamuzi wa hivi karibuni wa Bodi katika kesi ya Mwito wa Maandamano ya Wanawake wa Kuba, ambapo Bodi ilisisitiza kwamba kusoma chapisho katika muktadha inapaswa kuzingatia hali ya uonevu wa serikali na mapendeleo makubwa ya umma katika maandamano ya kihistoria ambayo yalikuwa mada kuu za maandamano. Isitoshe, kampuni hiyo ilizingatia keshi ya Kauli Mbiu ya Maandamano ya Iran, ambapo Bodi ilichambua vuguvugu la kisiasa lililokuwa likipigania haki za wanawake nchini Iran. Hapo, Bodi ilisisitiza umuhimu wa kulinda sauti katika muktadha wa vuguvugu la maandamano, hususan kuhusiana na uonevu wa kimfumo wa serikali ya Iran dhidi ya uhuru wa kujieleza na umuhimu wa nafasi za kidijitali kama jukwaa la kuonyesha upinzani. Kampuni hiyo ilibainisha kwamba ilikuwa imezingatia uamuzi wa hivi karibuni wa muhtasari katika kesi ya Kauli ya Kimafumbo Dhidi ya Rais wa Peruu, ambayo ilisisitiza tena “umuhimu wa kuunda mifumo ya uratibu inayozingatia muktadha na kufahamu kuhusu kinaya, kejeli au semi za balagha, hususan ili kulinda kauli za kisiasa.”
Viwango vya Jumuiya kuhusu Kupanga Madhara na Kuendeleza Uhalifu
Meta ilifahamisha Bodi kwa pia ilizingatia kuondoa maudhui hayo chini ya Viwango vya Jumuiya kuhusu Kupanga Madhara na Kuendeleza Uhalifu kwa kufichua utambulisho wa mwanamke anayeonyeshwa kwenye video bila hijabu bila idhini yake. Meta hutekeleza mkondo huu wa sera ikiwa tu kesi imepelekwa katika kiwango kingine na muktadha zaidi ukatolewa. Utekelezaji unahitaji mchango wa washikadau wafaao na unalenga kubaini iwapo maudhui yanaonyesha mwanamke asiye na hijabu, kufichua utambulisho wake bila idhini yake na uwezekano wa kumweka hatarini, badala ya istilahi zozote mahususi zilizotumika au toni ya maudhui au manukuu. Meta inabainisha kuwa mtu hawezi “kujifichua” mwenyewe – kitendo cha kifichua utambulisho ni sharti kiwe ambacho mtu hajaridhia ili kukiuka sera.
Katika kesi hii, Meta ilibaini kuwa maudhui husika hayapaswi kuondolewa kwa kufichua utambulisho bila idhini kwa sababu utambulisho wa mwanamke huyo unajulikana pakubwa na unapatikana mtandaoni, na tayari amekamatwa kufikia wakati ambapo maudhui ya kesi hii yalichapishwa. Muktadha huu ulipunguza pakubwa hatari ya madhara yanayohusishwa na kuondoa maudhui hayo kwenye jukwaa.
Bodi iliuliza Meta maswali 11 na maswali mawili ya kufuatilia katika maandishi. Maswali yanayohusiana na taratibu na nyenzo za utekelezaji za Iran, Tathmini ya Meta ya hatari nchini Iran kwa jumla na kwa mwanamke aliye kwenye video hasa, michakato otomatiki na ukaguzi wa binadamu, utekelezaji wa maudhui yanayoonyesha mwanamke asiyejifunika na ufichuzi wa utambulisho wa kikundi kilicho hatarini, katika kiwango au baada ya kupendekezwa kwa viwango vingine. Meta ilijibu maswali yote.
7. Maoni ya Umma
Bodi ya Usimamizi ilipokea maoni 12 ya umma yanayohusiana na kesi hii. Maoni saba kati ya hayo yaliwasilishwa kutoka Marekani na Kanada, mawili kutoka Asia ya Kati na Kusini, mawili kutoka Ulaya na moja kutoka Mashariki ya Kati na Afrika Kaskazini.
Mawasilisho yalishughulikia mada zifuatazo: nafasi ya mitandao ya kijamii katika maandamano ya Iran, ikiwa ni pamoja na vuguvugu la “Mwanamke, Maisha, Uhuru” na nafasi ambayo picha ya wanawake ambao hawajajifunika kwa hijabu inachukua katika kampeni za kidijitali; hatari za kusambaza picha zinazoonyesha wanawake wasiojifunika kwa hijabu kwenye mitandao ya kijamii nchini Iran; matumizi ya mitandao ya kijamii na mamlaka za Iran; Utekelezaji wa Meta wa sera zake za uratibu wa maudhui kauli ya lugha ya Kiajemi inayohusiana na hali ya kisiasa nchini Iran, uhuru wa kujieleza, haki za binadamu, haki za wanawake, uonevu wa serikali na marufuku dhidi ya mitandao ya kijamii nchini Iran.
Ili kusoma maoni ya umma yaliyowasilishwa kuhusu kesi hii, tafadhali bofya hapa.
8. Uchanganuzi wa Bodi ya Usimamizi
Bodi ilitathmini uamuzi wa kwanza wa Meta wa kuondoa maudhui chini ya sera ya maudhui, wajibu wa haki za binadamu na maadili ya kampuni hiyo.
Bodi ilichagua kesi hii kwa sababu ilitoa fursa ya kuchunguza sera za Meta dhidi ya Vurugu na Uchochezi pamoja na Kupanga Madhara na Kuendeleza Uhalifu, na vilevile michakato inayohusiana ya utekelezaji katika muktadha wa maandamano makubwa kutetea haki za wanawake na kushiriki kwa wanawake katika shughuli za umma nchini Iran tangu Septemba 2022. Hasa, inashughulikia umuhimu wa mitandao ya kijamii kwa watu wanaoandamana dhidi ya kanuni za lazima za kuvaa hijabu.
Vilevile, kesi hii inaipa Bodi fursa ya kujadili taratibu za ndani za Meta zinazobaini wakati na kwa nini kauli za kimafumbo, ambazo, zikieleweka kwa njia halisi, zinaweza kufasiriwa kuwa za kutishia, lakini ambayo kutokana na muktadha hazipaswi kufasiriwa kama tishio la kusadikika. Kesi hiyo kimsingi inawekwa katika kipaumbele cha Bodi cha Uchaguzi na Nafasi za Kiraia, lakini pia inagusia vipaumbele vya Bodi vya Jinsia, Serikali Kutumia Majukwaa ya Meta na Hali za Janga na Migogoro.
8.1 Utiifu wa Sera za Maudhui za Meta
Kiwango cha Jumuiya kuhusu Vurugu na Uchochezi
Bodi imepata kwamba maudhui katika kesi hii hayakiuki Viwango vya Jumuiya kuhusu Vurugu na Uchochezi kwa kuwa yana kauli ya kimafumbo yanayoeleza hasira dhidi ya uonevu wa serikali, badala ya ufasiri sisisi na hivyo kuwa tishio la kusadikika la vurugu.
Meta ilieleza kwamba awali iliondoa maudhui katika kesi hii kwa sababu yana “taarifa ya nia ya kutekeleza vurugu za ubaya wa juu.” Inafafanua vurugu za ubaya wa juu kama tishio ambalo linaweza kusababisha kifo au linaweza kusababisha mauaji.
Kulingana na tathmini ya timu zake za kikanda, Meta ilifasiri kauli “haipo mbali na kukufanya kuwa vipande” kutoka kwenye manukuu ya chapisho hilo kuwa tishio la madhara ya kimwili katika muktadha wa Iran, hali inayokiuka sera ya Vurugu na Uchochezi.
Wataalamu wa kiisimu ambao Bodi itafuta ushauri wao walieleza kwamba sehemu muhimu ya manukuu hayo yanaweza kutafsiriwa kama “hivi karibuni tutakurua kwa vipande!” au “hivi karibuni, tutakufanya kuwa vipande vidogo.” Wataalamu walibaini kwamba kauli katika muktadha wa Iran inaonyesha hasira, kutamauka na chuki dhidi ya wadhalimu na kupendekeza wazo kwamba hali hatimaye zinaweza kubadilika kwa sababu wadhalimu hawashikilia uongozi milele. Kauli hii haipaswi kufasiriwa kwa njia sisisi kama nia ya kusababisha madhara ya kimwili; badala yake, inatumika kama “taarifa ya balagha” inayolenga kuvutia makini, inayosisitizwa kupitia lugha yenye hisia nzito inayohusisha vitenzi vya kushurutisha kama vile “rarua” au “rarua kuwa vipande/vipande vidogo.” Wataalamu hawa waliangazia kwamba kauli kama hizi za kimafumbo zinaakisi hasira ya kina inayoonyeshwa na mtumiaji aliyechapisha maudhui haya pamoja na hadhira yake. Kwa hivyo, haihusu matishio halisi ya vurugu halisi za kimwili.
Ingawa Meta ilifahamisha Bodi kwamba pia inazingatia muktadha wa kauli inapotathmini iwapo tishio ni la kusadikika, mwongozo wake kwa waratibu hauashirii kwamba wanaweza kuzingatia muktadha wanapotathmini ikiwa kuna “taarifa ya nia [kutekeleza] vurugu za ubaya wa juu.” Ilimradi vipengele vya kanuni vimetimizwa, hususan maudhui yakiwa na tishio pamoja na mlengwa, chapisho linapatikana kuwa la ukiukaji, kama ilivyo katika kesi hii. Katika kesi hii, Meta ilifasiri taarifa hiyo kuwa ya kulenga mwanaume anayemfuata mwanamke husika. Kanuni haihitaji mlengwa kuonekana au kuweza kutambuliwa. Kanuni inatoa mfano mmoja tu wa kauli ya kutishia ambayo ina kighairi au haizingatiwi kuwa tishio la kusadikika kama kanuni: “matishio yanayoelekezwa dhidi ya watendaji fulani wa vurugu, kama vile makundi ya kigaidi.”
Kauli “kukufanya kuwa vipande” hapa haitoshi kuwa tishio la kusadikika. Kutokana na muktadha wa kipindi cha msukosuko, ongezeko la uonevu na vurugu dhidi ya waandamanaji dhidi ya utawala nchini Iran na kwa kuzingatia manukuu na video nzima, Bodi imepata kwamba kauli hii ni ya kimafumbo, si halisi, inayoonyesha hasira na fazaa na serikali, na haitoshi kuwa “taarifa ya nia ya [kutekeleza] vurugu za ubaya wa juu.” Ufasiri huu unaambatana na ahadi ya Meta ya kutetea sauti, na umuhimu wa kulinda hali ya kuonyesha kutoridhika kisiasa.
Viwango vya Jumuiya kuhusu Kupanga Madhara na Kuendeleza Uhalifu
Bodi imegundua kuwa maudhui katika kesi hii hayakiuki Viwango vya Jumuiya kuhusu Kupanga Madhara na Kuendeleza Uhalifu.
Meta ilizingatia kuondoa chapisho hilo chini ya kanuni inayopiga marufuku “maudhui yanayoweka wanawake wasiovaa shela katika hatari ya kufichukua picha zao bila shela za kujifunika kinyume na matakwa au idhini yao.” Mkondo huu wa sera umehaririwa ili kupiga marufuku: “Kufichua utambulisho wa [wanawake wasio na shela]: kuweka peupe utambulisho wa mtu na kumweka katika hatari ya madhara.” Kampuni hii inaelewa “kufichua utambulisho” kujumuisha maudhui yanayoshiriki picha ya mwanamke asiya na shela, yanayoweka wazi utambulisho wake bila idhini yake na kumweka katika hatari ya madhara. Mkondo huu wa sera unatumika tu maudhui yanapopendekezwa kwa Bodi na huhitaji michango kutoka kwa washikadau mbalimbali ili kutekelezwa (angalia Sehemu ya 4 hapo juu).
Katika kesi hii, Bodi inakubaliana na Meta kwamba maudhui hayo “hayamfichui” mwanamke huyo, kwa sababu utambulisho wake ulikuwa unafahamika pakubwa na hatari ya madhara ilikuwa imezuiwa kwa sababu tayari alikuwa amekamatwa kufikia wakati ambapo maudhui hayo yalichapishwa. kwa hivyo, video hiyo kusalia kwenye jukwaa haingeongeza kiwango cha hatari kwa mwanamke huyo na hakika kungemlinda kwa kutoa uhamasisho kuhusu kesi yake. Kubaini iwapo chapisho “linafichua utambulisho” wa mwanamke na kumweka katika hatari hutegemea hasa muktadha; utekelezaji wa sera hii baada ya kupendekezwa kwa viwango vingine pekee unaweza kuhakikisha kuwa timu inayoitekeleza ina muda na nyenzo za kutambua na kuzingatia muktadha muhimu kwa ufanisi.
8.2 Uzingatiaji wa Wajibu wa Haki za Binadamu wa Meta
Bodi imegundua kuwa kuondoa maudhui kwenye jukwaa hilo kunaendana na majukumu ya haki za binadamu ya Meta.
Uhuru wa Kujieleza (Kifungu cha 19 cha ICCPR)
Kifungu cha 19 cha ICCPR kinabainisha ulinzi mpana wa uhuru wa kujieleza, ikiwa ni pamoja na “uhuru wa kutafuta, kupokea na kutoa maelezo na maoni ya kila aina, bila kujali vizuizi, iwe kwa maneno, maandishi au kwa chapisho, kwa njia ya sanaa, au kupitia media nyingine yoyote anayoipenda.” Ambapo serikali imeweka vikwazo dhidi ya usemi, vikwazo hivyo lazima vitimize masharti ya kutii sheria, lengo halali na umuhimu na ulinganifu (Kifungu cha 19, aya ya 3 ya ICCPR). Bodi hutumia mfumo huu kutafsiri ahadi za hiari za haki za binadamu za Meta, kuhusiana na uamuzi wa maudhui ya mtu binafsi unaokaguliwa na kile kinachosemwa na Meta kuhusu usimamizi wa maudhui. Kama vile Mjumbe Maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu uhuru wa kujieleza alivyosema, ingawa “kampuni hazina wajibu wa Serikali, aina ya athari zao huzihitaji kutathmini aina sawa ya maswali kuhusu kulinda hali za kujieleza huru za watumiaji wao,” ( A/74/486, aya ya 41).
Ufikiaji wa mtandao wa kijamii ni muhimu katika jamii funge kama ya Irani. Kama “walinzi wa kidijitali,” majukwaa ya mitandao ya kijamii yana “athari kubwa” kwa umma kufikia taarifa ( A/HRC/50/29, aya ya. 90). Chapisho kwenye kesi hii ni sehemu ya vuguvugu pana la maandamano linalotegemea nafasi za kidijitali za raia ili kukua. Sheria zinazobainisha jinsi wanawake lazima wavae huathiri uhuru na hadhi yao ( A/68/290, aya ya. 38), iwe sheria inalenga kupiga marufuku kuvaa shela au kukataza kutembea hadharani bila (tazama m.f., Yaker v France, CCPR/C/123/D/2747/2016). Kuhusiana na hilo, “Intaneti imekuwa uwanja mpya wa vita katika mapambano ya haki za wanawake, na kuongeza fursa kwa wanawake kujieleza,” ( A/76/258 aya ya 4). Kuwezesha wanawake kujieleza huru kunawawezesha kushiriki katika shughuli za kisiasa na kupata haki zao za binadamu ( A/HRC/Res/23/2, aya za 1-2; A/76/258, aya ya 5).
I. Uhalali (uwazi na upatikanaji wa sheria)
Kanuni ya uhalali inahitaji kizuizi chochote dhidi ya uhuru wa kujieleza kufuata sheria iliyowekwa, ambayo inaweza kufikiwa na ni wazi kwa watumiaji. Kanuni hiyo lazima “iundwe kwa usahihi wa kutosha ili kumwezesha mtu kudhibiti mienendo yake ipasavyo na ni lazima iweze kufikiwa na umma,” ( Maoni ya Jumla Nambari. 34, aya ya 25). Isitoshe, kanuni zinazozuia kujieleza “haziwezi kutoa uamuzi usiozuiliwa kwa kizuizi cha uhuru wa kujieleza kwa wale walioshtakiwa kwa utekelezaji [wao]” na “zitoe mwongozo wa kutosha kwa waliohukumiwa na utekelezaji wao ili kuwawezesha kuwa na uhakika kuhusu aina za usemi zimewekewa kikomo vizuri na aina zisizo na kikomo,” (Maoni ya Jumla Nambari 34, aya ya 25; A/HRC/38/35 (undocs.org), aya ya 46). Ukosefu wa uwazi au usahihi unaweza kusababisha kutofuatana na sheria kutekelezwa kiholela. Ilivyo kwa Meta, watumiaji wanapaswa kuwa na uwezo wa kubashiri madhara ya kuchapisha maudhui kwenye Facebook na Instagram, na wakaguzi wa maudhui wanapaswa kuwa na mwongozo ulio wazi kuhusu utekelezaji.
Kiwango cha Jumuiya kuhusu Vurugu na Uchochezi
Bodi imebaini kwamba ingawa mtazamo wa sera – ambao unaeleza malengo ya Viwango vya Jumuiya lakini si sehemu ya kanuni yenyewe – wa Viwango vya Jumuiya kuhusu Vurugu na Uchochezi unapendekeza kwamba “muktadha ni muhimu,” na unaweza kuzingatiwa wakati wa kutathmini “tishio la kusadikika,” miongozo ya ndani na mbinu za Meta za uratibu haziwezeshi hili katika utendaji. Jinsi Bodi ilivyobainisha kwenye kesi ya Kauli Mbiu ya Maandamano ya Irani, mratibu wa maudhui katika kiwango anaagizwa kuangalia vigezo mahususi, au vipengee, kwenye chapisho, na ilimradi vipengee hivyo vimetimizwa, waratibu wanaagizwa kuondoa chapisho husika. Yaani, ikiwa chapisho lina tishio (m.f., “ua” au “nitakurarua vipande”) na kuna mlengwa, matokeo yake ni kuondolewa. Waratibu wa maudhui hawajawezeshwa kufanya tathmini kuhusu iwapo tishio ni la kusadikika. Kama Meta ilivyoelezwa katika kesi hiyo, mbinu ya ukariri au kufuata fomula ni kwa sababu “kutathmini iwapo [kauli] ina kauli ya balagha wala si ya tishio la kusadikika ina changamoto, hususan katika kiwango.” Kuzingatia kusadikika kwa matishio kunafanywa katika kuunda kanuni, si kuitekeleza. Kama Bodi ilivyobainishwa katika kesi ya Kauli Mbiu ya Maandamano ya Irani ingawa “utaratibu wa sera unaonekana kukubali matamshi ya balagha ya aina ambayo yanaweza kutarajiwa katika miktadha ya maandamano, kanuni zilizoandikwa na mwongozo unaolingana kwa wakaguzi hazikubali. Kwa hakika, utekelezaji kwa vitendo, hasa kwa kiwango, ni wa kimfumo zaidi kuliko sheria zinavyodokeza, na hii inaweza kuunda maoni potofu kwa watumiaji kuhusu jinsi sheria zinavyoweza kutekelezwa. Mwongozo kwa wakaguzi, kama ilivyoandikwa kwa sasa, haujumuishi uwezekano wa uchanganuzi wa kimuktadha, hata kama kuna viashiria wazi ndani ya maudhui yenyewe kwamba lugha ya kutisha ni balagha.” Hali ya kutolingana kati ya mtazamo wa sera uliotajwa na kampuni na desturi zake halisi za utekelezaji inaendelea na haikidhi ipasavyo kanuni ya uhalali.
Bodi inasisitiza matokeo yake kutokana na kesi ya Kauli Mbiu ya Maandamano ya Irani kwamba Meta inapaswa kutoa mwongozo wenye hali zote kuhusu jinsi ya kuzingatia muktadha, kuelekeza waratibu kuepuka kuondoa lugha ya “balagha” au lugha isiyo halisi inayoeleza upinzani, hususan katika mazingira nyeti ya kisiasa, kama vile Iran.
Viwango vya Jumuiya kuhusu Kupanga Madhara na Kuendeleza Uhalifu
Bodi imepata kwamba marufuku ya Meta dhidi ya “maudhui yanayoweza wanawake wasio na shela katika hatari ya kufichua utambulisho wako bila shela kinyume na matakwa au bila idhini yao” si wazi, kama iliyotumika katika kesi hii. Inabainisha wazi kwamba maudhui “yanayofichua utambulisho” wa wanawake wasio na shela na yanaweza kusababisha madhara hayaruhusiwi kwenye majukwaa ya Meta. Hata hivyo, Bodi imebainisha kwa wasiwasi kwamba Miongozo ya Jumuiya haiunganishwi moja kwa moja na Viwango vya Jumuiya kuhusu Kupanga Madhara na Kuendeleza Uhalifu. Hali hii inahujumu hali ya ufikivu wa kanuni kwa watumiaji wa Instagram. Katika kesi za awali ( Dalili za Saratani ya Matiti na Picha za Uchi, Kutengwa kwa Öcalan), Bodi imependekeza kwamba Meta iweke wazi kwa umma ili watumiaji wafahamu jinsi Viwango vya Jumuiya ya Facebook vinatumika katika Instagram. Katika kujibu, Meta imefanya mchakato wa kuunganisha Viwango vya Jumuiya na Miongozo ya Jumuiya ya Instagram na kubainisha sehemu ambazo sera zinatofautiana kidogo kwenye majukwaa hayo. Katika kuhakikisha ripoti za kila robo mwaka za uwazi, Meta imeihakikishia Bodi kwamba juhudi hizi zinaendelea kupewa kipaumbele, ikibainishwa kwamba masuala ya kisheria na udhibiti yameathiri muda wao. Bodi inasisitiza umuhimu wa kuharakisha ili kukamilisha mchakato huu na kuhakikisha uwazi wa kanuni zinazotumika.
II. Lengo Halali
Chini ya Kifungu cha 19, aya ya 3 ya ICCPR, kauli inaweza kuwekewa vizuizi kwa sababu mahususi na zenye kikomo, ikiwa ni pamoja na madhumuni ya kulinda haki za wengine. Katika kesi hii, Bodi imepata kwamba Viwango vya Jumuiya kuhusu Unyanyasaji na Uchochezi vinalenga “kuzuia madhara yanayoweza kutokea nje ya mtandao” kwa kuondoa maudhui ambayo yanaleta “hatari halisi ya madhara ya kimwili au vitisho vya moja kwa moja kwa usalama wa umma.” Sera hii kwa hivyo inatimiza lengo halali la kulinda haki ya maisha na haki ya usalama wa mtu (Kifungu cha 6, ICCPR) na haki ya usalama wa kimwili wa mtu (Kifungu cha 9 cha ICCPR; Maoni ya Jumla Nambari 35, aya ya 9).
Sera dhidi ya Kupanga Madhara na Kuendeleza Uhalifu inatekeleza lengo halali la kulinda haki ya wanawake nchini Irani dhidi ya kubaguliwa (Vifungu vya 2, 3 na 26, ICCPR; Vifungu vya 1 na 7, CEDAW), ikiwa ni pamoja na kufurahia hali ya uhuru wa kujieleza na kukutana (Vifungu vya 19 na 21, ICCPR), haki ya kushiriki katika shughuli za umma (Vifungu vya 1 na 7, CEDAW), haki ya faragha (Kifungu cha 17, ICCPR) na haki zao za maisha (Kifungu cha 6, ICCPR ) na uhuru na usalama wa mtu (Kifungu cha 9 ICCPR).
III. Umuhimu na Uwiano
Vizuizi vyovyote vya uhuru wa kujieleza “lazima viwe muhimu ili kufikia utendakazi wao wa ulinzi; lazima viwe chombo cha ukali wa chini zaidi miongoni mwa vile vyote vinavyoweza kufikia utendakazi wao wa ulinzi; lazima vilingane na masilahi yanayopaswa kulindwa,” (Maoni ya Jumla Nambari 34, aya ya 34). Kampuni za mitandao ya kijamii zinapaswa kuzingatia aina mbalimbali za majibu yanayowezekana kwa maudhui yenye matatizo ambayo hayawezi kufutwa ili kuhakikisha kuwa vizuizi vinapunguzwa ( A/74/486 aya ya 51).
Kiwango cha Jumuiya kuhusu Vurugu na Uchochezi
Bodi ilibaini kuwa uamuzi wa kwanza wa Meta wa kuondoa maudhui katika kesi hii haukuwa muhimu. Haukuhitajika ili kulinda usalama wa mtu aliyekuwa akirekodi video au watu wengine, kwa kuwa tishio lililotajwa kwenye manukuu ya chapisho si halisi. Bodi ina wasiwasi kwa hata baada ya mwongozo wake katika kesi ya Kauli Mbiu ya Maandamano ya Irani, Viwango vya Jumuiya na mwongozo wa kampuni hiyo uliotolewa na waratibu bado unaacha mwanya wa utekelezaji usiolinganifu wa matisho ya kimafumbo (yasiyo halisi), licha ya hali nchini Irani, huku maandamano yakiendelea kwa zaidi ya mwaka mmoja sasa. Kesi hiyo, sawa na hii, ilihusisha kauli ambayo Meta ilikosa kutambua kama taarifa ya tishio lisilo halisi. Kuendelea kukosa mwongozo wa kutosha kumezidi kuangaziwa na ukweli kwamba maudhui katika kesi hii yalikaguliwa na waratibu wengi katika kiwango na timu za ndani ya Meta, na mara kwa mara kupatikana kuwa yalikuwa ya ukiukaji.
Kama sehemu ya uchambuzi wake, Bodi ilichukua sababu sita kutoka kwenye Mpango wa Utekelezaji wa Rabat ili kutathmini uwezo wa maudhui katika kesi hii kusababisha hatari kubwa ya kuchochea ubaguzi, vurugu au hatua zingine zisizofuata sheria. Bodi inabainisha kuwa ingawa vigezo vya Rabat viliundwa kwa ajili ya utetezi dhidi ya chuki ya kitaifa, kikabila au kidini ambayo ni sehemu ya uchochezi, na si kwa uchochezi kwa jumla, jaribio la vigezo sita ni muhimu katika kutathmini uchochezi kwa jumla, na Bodi imeitumia kwa njia hii hapo awali (tazama, kwa mfano, Kauli Mbiu ya Maandamano ya Iran na Mwito wa Maandamano ya Wanawake nchini Kuba):
- Muktadha: Maudhui hayo yalichapishwa mmano Julai 2023, katika kipindi cha msukosuko, kuongezeka kwa uonevu na vurugu dhidi ya waandamanaji waliokuwa wakipinga utawala. Kuna njia chache za maandamano ndani ya nchi, kutokana na kukatizwa pakubwa kwa intaneti na kupigwa marufuku kwa majukwaa makuu ya mitandao ya kijamii kama vile Facebook, Telegram na X. Instagram ikiwa ndiyo mojawapo ya majukwaa machache yaliyosalia, nafasi yake katika vuguvugu la “Mwanamke, Maisha, Uhuru” haina kipimo. Wataalamu ambao Bodi ilitafuta ushauri wao walibaini kwamba vuguvugu hili linalenga kufanya kuwa jambo la kawaida maandamano na upinzani dhidi ya miongo minne ya sheria za ubaguzi dhidi ya wanawake. Wataalamu hao waligundua kuwa tangu kuanza kwa vuguvugu hilo, visa vya kuwatia hofu na kuwanyamazisha wanawake dhidi ya kujieleza mtandaoni vimeongezeka. Sheria mpya na kukamatwa kwa watu mashuhuri kunalenga kukandamiza maandamano haya na kukomesha hali ya kufanya kuwa jambo la kawaida upinzani wa sheria za hijabu.
- Utambulisho wa mzungumzaji: Meta ilifahamisha Bodi kwamba kampuni hiyo haikuzingatia mtumiaji aliyechapisha maudhui hayo kuwa mtu maarufu. Kulingana na manukuu yaliyo kwenye video, mtumiaji anaonekana kuwa mfuasi wa au sehemu ya vuguvugu la “Mwanamke, Maisha, Uhuru.” Kwa hivyo, mzungumzaji hapa hayupo katika nafasi ya mamlaka na pia ana uwezekano wa kuweka usalama wake hatarini kwa kuonyesha uungaji mkono na kuchapisha maudhui haya.
- Kusudi: Ingawa kutathmini nia wakati wa kuratibu maudhui katika kiwango kuna changamoto kuu, tafsiri yakinifu na ya kawaida ya chapisho nzima inaonyesha uungaji mkono wa mwanamke anayeonyeshwa na kutoa uhamasisho kuhusu kukamatwa kwake. Kulingana na wataalamu ambao Bodi ilitafuta ushauri wao, ni jambo la kawaida nchini Iran kwa waandamanaji kuzungusha picha ya mwanamke asiye na shela na jina lake kufuatia kukatwa kwake, ili kushinikiza mamlaka kumlinda. Waandamanaji wamejifunza kuwa kwa kutangaza watu hawa hadharani, wanaweza kuzuia unyanyasaji zaidi wa wahasiriwa.
- Maudhui na namna ya kujieleza: Kulingana na wataalamu wa isimu ambao Bodi ilishauriana nao, kauli “kufanya kuwa vipande” katika muktadha huu kunaweza kueleweka na wazungumzaji wa Kiajemi kuwa kueleza hisi nzito, kama vile hasira na kutamaushwa, lakini si tishio halisi la kusadikika la vurugu. Vuguvugu imetumia mara kwa mara lugha ya lazima na ya kutishia ili kunena dhidi ya utawala. Katika kesi ya Kauli Mbiu ya Maandamano ya Iran, Bodi ilipata kwamba kauli “Kifo kwa Khamenei” ilikuwa ni “balagha yenye tishio” na ikabainishwa kuwa Meta ilikuwa imetoa posho ya “nia ya sera” kwa kauli “Nitamuuwa yeyote atakayemuuwa dadangu/kakagu” kwa sababu sawa na hizo. Kauli katika kesi hii huonekana katikati ya manukuu yanayomsifu mwanamke ambaye alisimama kutetea haki zake. Yakizingatiwa kijumla, manukuu haya yanaonyesha uungaji mkono wa mwanamke wa Iran anayepinga sheria za kibaguzi na desturi za dhuluma za utawala.
- Kiwango na ufikiaji: Chapisho hilo lilikuwa limetazamwa mara 47,000, likapendwa mara 2,000, maoni 100 na kushirikiwa mara 50. Kutokana na kauli hii haikuonekana kuwa ya uchochezi kwa kuzingatia vigezo vingine kwenye uchambuzi wa Rabat, ufikiaji wa juu wa maudhui wenyewe si kigezo kinachoashiria kuwa uondoaji ulihitajika.
- Uwezekano na wepesi: Kigezo hiki hutathmini iwapo kauli ina uwezekano wa kuchochea uwezekano wa madhara na kwa wepesi dhidi ya anayeweza kuwa mlengwa wa kauli, ambaye katika kesi hii ilikuwa utawala. Vuguvugu la maandamano na wafuasi wake wanapigana dhidi ya utawala ambayo inatumia uonevu wa vurugu na ulipizaji kisasi dhidi ya waandamanaji. Namna ya madhara inayoweza kutokana na kauli hii ni vurugu za ulipizaji kisasi kutoka kwa utawala dhidi ya mtumiaji anayechapisha au mwanamke anayeonyeshwa kwenye video badala ya vurugu dhidi ya utawala au wafuasi wake. Wataalamu walisisitiza hatari zinazowakumba watu wanaoshiriki katika maandamanao haya, na jinsi ya vuguvugu hilo linavyostahimili licha ya tishio lililopo ya vurugu. Pia wanasema kwamba lengo la kusambaza picha za mwanamke asiye na shela ambaye amekamatwa ni kuvuta makini kuhusu kukamatwa kwake na kushinikiza mamlaka kumlinda.
Kulingana na uchanganuzi wa vigezo vilivyo hapa juu, Bodi inazingatia kwamba maudhui haya hayakuwa ya tishio la kusadikika na hayakuwa na uwezo wa kuchochea madhara ya nje ya mtandao. Kauli ya kimafumbo inapotumiwa katika muktadha wa maandamano makubwa yanayokumbwa na uonevu wa vurugu, Meta inapaswa kuwezesha wakaguzi wake kutathmini lugha na muktadha wa ndani, kuoanisha mwongozo kwa waratibu na mtazamo mkuu wa sera. Kuhakikisha tathmini sahihi ya iwapo chapisho ni “kauli ya kimafumbo” au likiwa na uwezekano wa kuchochea vurugu ni muhimu katika kuboresha uratibu katika janga kwa upana zaidi. Usahihi wa mifumo otomatiki utaathiriwa na ubora wa data ya mafunzo iliyotolewa na waratibu binadamu. Pale ambapo waratibu binadamu wanaondoa kauli za “kimafumbo” kutokana na utekelezaji mgumu wa kanuni, kosa hilo linaweza kutokea tena na kuongezwa kupitia kufanya mambo kiotomatiki.
Bodi inapobaini kwamba Meta ina mbinu kadhaa zinazopatikana za kurekebisha sera zake na utekelezaji wake katika hali za janga, ikiwa ni pamoja na mfumo wa viwango vya nchi “zilizo hatarini” na Itifaki yake ya Sera ya Janga. Mfumo wa viwango vya nchi “zilizo hatarini”hutumiwa kutambua nchi zilizo katika hatari ya “madhara ya nje ya mtandao na vurugu” ili kubaini jinsi kampuni hiyo inapaswa kutoa kipaumbele uundaji wake wa bidhaa au jinsi ya kuwekeza rasilimali zake. Tathmini hii inaweza kuzingatiwa katika michakato mingine (m.f., iwapo itatumia timu yake ya shughuli maalum au kuchochea matumizi ya Itifaki ya Sera ya Janga). Meta ilifahamisha Bodi kwamba katika nusu ya pili ya 2023, Iran imebainishwa kuwa “nchi iliyo katika hatari.” Iran pia imebainishwa chini ya Itifaki ya Sera ya Janga tangu Septemba 21, 2022, na imeendelea kubainishwa tangu wakati huo. Itifaki ya Sera ya Janga inawezesha Meta kufanya mabadiliko fulani ya muda, yanayojulikana na “nyenzo za sera,” ili kutatua hali fulani mahususi. Meta imetoa baadhi ya mifano ya nyenzo za sera ambazo tayari zinatumika nchini Iran, ikiwa ni pamoja na “posho inayoruhusu maudhui yanayojumuisha kauli kwamba 'nitamuuwa yeyote atakayemuuwa dadangu au kakangu' au kauli zitokanazo na hiyo, bila ukiukaji mwingine wa sera zetu.” (Ili upate mifano ya nyenzo za sera, tazama Madokezo ya Mkutano kuhusu Sera, Januari 25, 2022, Itifaki ya Sera ya Janga.)
Ingawa Bodi inatambua kujitolea kwa kampuni kudumisha usalama na juhudi zake za kukabiliana na hatari zinazoweza kuwepo za uratibu wa maudhui kwa kuamilisha Itifaki ya Sera ya Janga nchini Iran, juhudi hizi hazijatosha katika kuhakikisha heshima kwa uhuru wa watu kujieleza na kukutana katika mazingira ya uonevu wa kimfumo ya upinzani na taharuki za kijamii. Utafiti ulioendeshwa na Bodi unaashiria kiasi kikubwa sana cha maudhui yanayoonyesha wanawake bila shela katika muktadha wa kujadili mavazi ya hijabu nchini Iran, kwenye majukwaa ya Meta, hushirikiwa na au kuunga mkono vuguvugu la maandamano. Hapa, mchakato wa utekelezaji wa Meta imekosa mara kwa mara kupambanua taarifa za kimafumbo, au zisizo halisi, katika muktadha ufaao tofauti na matishio halisi na uchochezi wa vurugu, hali ambayo inaweza kuongeza madhara ya nje ya mtandao.
Bodi inapendekeza kwamba Meta iongeze nyenzo ya sera kwenye Itifaki ya Sera ya Janga, na kutoa utaratibu ufaao wa ndani kwa waratibu katika kiwango kuhusu jinsi ya kutambua taarifa zinazotumia lugha ya mafumbo yenye tishio, au kwa njia isiyo halisi, katika muktadha ufaao wa kuchukuliwa kuwa usio wa ukiukaji wa mkondo wa sera dhidi ya Vurugu na Uchochezi unaopiga marufuku matishio ya vurugu. Katika kuunda taratibu mahususi kwa janga kuhusu jinsi ya kubaini iwapo tishio ni la kimafumbo au si halisi, Meta inaweza kuangazia vigezo vya Mpango wa Rabat (m.f., muktadha wa maandamano makubwa dhidi ya uonevu wa serikali, iwapo mzungumzaji ana uwezo wa kuchochea au anawakilisha hatari ya kuchochea watu kushiriki katika madhara, muktadha muhimu wa kiisimu na kijamii unaoashiria matumizi ya kawaida ya lugha kali/ yenye hisia nzito kwa nguvu ya balagha, uwezekano wa madhara kutokana na ufahamu wa eneo husika, n.k). Kampuni pia inaweza kutegemea washirika wake inayowaamini kusaidia kubuni au kutathmini utaratibu wa uratibu. Meta yenyewe imesisitiza umuhimu halisi wa Mpango wa Hatua wa Rabat katika uratibu wa maudhui, baada ya kusaidia Umoja wa Mataifa katika kutafsiri Mpango wa Hatua katika lugha 32. Wenzo huu wa sera unapaswa kuruhusu “kauli ya kimafumbo” katika muktadha wa maandamano dhidi ya utawala, ilimradi haina nia na hakuna uwezekano kwamba, zitachochea vurugu.
Viwango vya Jumuiya kuhusu Kupanga Madhara na Kuendeleza Uhalifu
Katika kesi hii, Bodi imepata uondoaji chini ya Viwango vya Jumuiya kuhusu Kupanga Madhara na Kuendeleza Uhalifu kuwa si muhimu, kwa kuwa mwanamke aliyetambuliwa anafahamika sana na maudhui hayo bila shaka yalichapishwa ili kutoa habari za kukamatwa kwake, kwa matumaini kwamba habari hizo zingesababisha aachiliwe huru. Isitoshe, watu wengi waliotoa maoni ya umma waliangazia kwamba mwanamke ambaye aliondoa hijabu hadharani alifanya hivyo kimakusudi, kama njia ya upinzani na anafahamu kuhusu madhara yanayoweza kutokea, kuchagua “ukaidi kama upinzani wa kimkakati dhidi ya mamlaka,” (angalia maoni ya umma ya Taasisi ya Tech Global, PC-21009). Mwanamke kwenye video hii tayari alikuwa ametambuliwa na kukamatwa na utawala. Chapisho hili lilishiriki ili kutoa habari kuhusu kukamatwa kwake. Waandamanaji na wapinzani waliofungwa na utawala wamepitia mateso, dhuluma za kijinsia au kutoweka. Wataalamu ambao Bodi itafuta ushauri wao na watu wengi walitoa maoni ya umma walibainisha kwa njia mahususi kwamba desturi hii, kutoa mwito wa kukamatwa na kutoa mwito wa kuachiliwa kwa mtu aliyefungwa, hutumiwa mara kwa moja na vuguvugu na watetezi wa haki za binadamu nchini Iran, na inaweza kusaidia kuwalinda watu waliozuiliwa na utawala.
Kusawazisha hitaji la kulinda utambulisho wa watumiaji walio hatarini huku tukiepuka kudhibiti wale wanaotaka kuonekana ni hoja inayohitaji uangalifu mkubwa na uchambuzi wa kimuktadha, ukaguzi kwa wakati ufaao na hatua ya haraka.
9. Uamuzi wa Bodi ya Usimamizi
Bodi ya Usimamizi imebatilisha uamuzi wa awali wa Meta wa kuondoa maudhui hayo.
10. Mapendekezo
- Utekelezaji
Ili kuhakikisha kuwa uhuru wa watumiaji kujieleza na kukutana unaheshimiwa katika mazingira ya uonevu wa kimfumo wa serikali, Meta inapaswa kuweka wenzo wa sera kwenye Itifaki ya Sera ya Janga unaosema kwamba taarifa za mafumzo (zisizo halisi), zisizonuiwa na hazina uwezekano wa kuchochea vurugu, hazikiuki mkondo wa sera ya Vurugu na Uchochezi unaopiga marufuku matishio ya vurugu katika miktadha inayofaa. Hii inapaswa kujumuisha kuunda vigezo kwa waratibu wa kiwango kuhusu jinsi ya kutambua kauli kama hizi katika muktadha husika.
Bodi itazingatia kuwa pendekezo hili limetekelezwa wakati Meta itashiriki na Bodi mbinu za utekelezaji wa wenzo wa sera na utaratibu utakaofuata katika uratibu nchini Iran.
*Dokezo la Kiutaratibu:
Maamuzi ya Bodi ya Usimamizi yanatayarishwa na majopo ya Wanachama watano na kuidhinishwa na wengi wa wanachama wa Bodi. Maamuzi ya Bodi hayawakilishi maoni ya kibinafsi ya Wanachama wote.
Kwa uamuzi wa kesi hii, utafiti huru ulipangwa kwa niaba ya Bodi. Bodi ilisaidiwa na taasisi huru ya utafiti yenye makao yake makuu katika Chuo Kikuu cha Gothenburg, ambayo inashirikisha timu ya zaidi ya wanasayansi wa kijamii 50 kutoka mabara sita, pamoja na zaidi ya wataalamu 3,200 wa kila nchi kutoka kote ulimwenguni. Bodi pia ilisaidiwa na Duco Advisors, shirika la ushauri linalolenga miingiliano ya siasa za ulimwengu, uaminifu na usalama na teknolojia. Memetica, shirika ambalo linajihusisha na utafiti wa chanzo huria kuhusu mienendo ya mitandao ya kijamii, pia ilitoa uchanganuzi. Utaalam wa lugha ulitolewa na Lionbridge Technologies, LLC, ambayo wataalamu wake wanajua lugha zaidi ya 350 na hufanya kazi kutoka miji 5,000 ulimwenguni kote.